19
Waisraeli Kwenye Mlima Sinai
Mnamo mwezi wa tatu baada ya Waisraeli kuondoka Misri, siku kama iyo hiyo, wakafika katika Jangwa la Sinai. Baada ya kuondoka Refidimu, waliingia katika Jangwa la Sinai na Israeli wakapiga kambi pale jangwani mbele ya mlima.
Kisha Mose akakwea kwenda kwa Mungu, naye Bwana akamwita kutoka kwenye ule mlima akasema, “Hivi ndivyo utakavyosema na nyumba ya Yakobo na utakachowaambia watu wa Israeli: ‘Ninyi wenyewe mmeona nililofanya huko Misri, jinsi nilivyowabeba kwenye mbawa za tai na kuwaleta kwangu. Sasa kama mkinitii kikamilifu na kutunza Agano langu, basi ninyi mtakuwa mali yangu ya thamani kubwa miongoni mwa mataifa yote. Ijapokuwa dunia yote ni mali yangu, ninyi mtakuwa kwangu ufalme wa makuhani na taifa takatifu.’ Haya ndiyo maneno utakayosema kwa wana wa Israeli.”
Kwa hiyo Mose akarudi, akawaita wazee wa watu na kuwaambia maneno yote ambayo Bwana alikuwa amemwamuru ayaseme. Watu wote wakajibu kwa pamoja, “Tutafanya kila kitu Bwana alichokisema.” Naye Mose akarudisha majibu yao kwa Bwana.
Bwana akamwambia Mose, “Nitakujia katika wingu zito, ili watu wanisikie nikinena nawe na kila mara waweke tumaini lao kwako.” Kisha Mose akamwambia Bwana yale ambayo watu walikuwa wamesema.
10 Naye Bwana akamwambia Mose, “Nenda kwa watu ukawaweke wakfu leo na kesho. Waambie wafue nguo zao 11 na wawe tayari siku ya tatu, kwa sababu siku hiyo, Bwana atashuka juu ya mlima Sinai machoni pa watu wote. 12 Weka mipaka kuzunguka mlima kwa ajili ya watu, uwaambie, ‘Mwe waangalifu, msije mkapanda mlimani au kuugusa. Yeyote atakayeugusa mlima hakika atauawa. 13 Hakika atapigwa mawe au kupigwa mishale; mkono wa mtu hautamgusa. Akiwa mwanadamu au mnyama, hataruhusiwa kuishi.’ Ila tu wakati baragumu itakapopigwa kwa mfululizo, ndipo watu wote watakapopanda mlimani.”
14 Baada ya Mose kushuka kutoka mlimani akawaendea watu na kuwaweka wakfu, wakafua nguo zao. 15 Kisha akawaambia watu, “Jitayarisheni kwa ajili ya siku ya tatu. Mwanaume yeyote asimkaribie mwanamke.”
16 Asubuhi ya siku ya tatu kulikuwa na ngurumo na radi pamoja na wingu nene juu ya mlima na mlio mkubwa sana wa tarumbeta. Kila mmoja aliyekuwa kambini akatetemeka. 17 Kisha Mose akawaongoza watu kutoka kambini kukutana na Mungu, nao wakasimama chini ya mlima. 18 Mlima Sinai ulikuwa umefunikwa na moshi, kwa sababu Bwana alishuka juu yake katika moto. Moshi wa moto huo ulipanda juu kama moshi kutoka kwenye tanuru kubwa na mlima wote ukatetemeka kwa nguvu nyingi, 19 nayo sauti ya tarumbeta ikawa kubwa zaidi na zaidi. Kisha Mose akazungumza na sauti ya Bwana ikamjibu.
20  Bwana akashuka juu ya Mlima Sinai na akamwita Mose apande juu mlimani. Kwa hiyo Mose akapanda juu, 21 naye Bwana akamwambia Mose, “Shuka ukawaonye watu ili wasijipenyeze kutafuta kumwona Bwana na wengi wao wakafa. 22 Hata makuhani, watakaomkaribia Bwana ni lazima wajiweke wakfu, la sivyo Bwana atawaadhibu.”
23 Mose akamwambia Bwana, “Watu hawawezi kupanda mlima Sinai kwa sababu wewe mwenyewe ulituonya ukisema, ‘Wekeni mipaka kuuzunguka mlima na kuutenga kama patakatifu.’ ”
24  Bwana akajibu, “Shuka ukamlete Aroni pamoja nawe. Lakini makuhani pamoja na watu wasije wakalazimisha kuja kwa Bwana, nisije nikawaadhibu.”
25 Basi Mose akashuka kwa watu na kuwaambia lile aliloambiwa.