33
Yakobo akutana na Esau
1 Yakobo akainua macho, akamwona Esau akija na watu wake mia nne. Kwa hiyo akawagawanya watoto kati ya Lea, Raheli na wale wajakazi wake wawili.
2 Akawaweka wale wajakazi na watoto wao mbele, Lea na watoto wake wakafuata, nao Raheli na Yusufu wakaja nyuma.
3 Yeye mwenyewe akatangulia mbele na kusujudu hadi chini mara saba alipomkaribia ndugu yake.
4 Lakini Esau akamkimbilia Yakobo kumlaki na kumkumbatia, akamwangukia shingoni na kumbusu. Nao wakalia.
5 Esau akainua macho, akawaona wale wanawake na watoto. Akauliza, “Hawa waliofuatana nawe ni nani?”
Yakobo akamjibu, “Ni watoto ambao Mungu amempa mtumishi wako kwa neema.”
6 Kisha wale wajakazi na watoto wao wakakaribia na kusujudu.
7 Kisha Lea na watoto wake wakaja na kusujudu. Mwisho wa wote wakaja Yusufu na Raheli, nao pia wakasujudu.
8 Esau akauliza, “Makundi hayo yote niliyokutana nayo yana maana gani?”
Akasema, “Ni ili kupata kibali machoni pako, bwana wangu.”
9 Lakini Esau akamwambia, “Ndugu yangu, tayari nina wingi wa mali. Ulivyo navyo viwe vyako mwenyewe.”
10 Yakobo akasema, “La hasha! Tafadhali, kama nimepata kibali machoni pako, upokee zawadi hii kutoka kwangu. Kwa maana kuuona uso wako ni kama kuuona uso wa Mungu, kwa kuwa umenipokea kwa kibali kikubwa.
11 Tafadhali kubali zawadi iliyoletwa kwako, kwa kuwa Mungu amenineemesha na ninavyo vyote ninavyohitaji.” Kwa sababu Yakobo alisisitiza, Esau akapokea.
12 Ndipo Esau akasema, “Tuendelee na safari; nitakusindikiza.”
13 Lakini Yakobo akamwambia, “Bwana wangu, unajua kwamba watoto ni wachanga na kwamba ni lazima nitunze hawa ng’ombe na kondoo wanaonyonyesha. Wakipelekwa kwa haraka hata kama ni kwa siku moja tu, wanyama wote watakufa.
14 Hivyo bwana wangu, mtangulie mtumishi wako, nami nije polepole kwa mwendo wa makundi yaliyo mbele yangu na mwendo wa watoto, hadi nifike kwa bwana wangu huko Seiri.”
15 Esau akamwambia, “Basi kubali nikuachie baadhi ya watu wangu.”
Yakobo akauliza, “Lakini kwa nini ufanye hivyo? Niache tu nipate kibali machoni pa bwana wangu.”
16 Hivyo siku hiyo Esau akashika njia, akarudi Seiri.
17 Pamoja na hayo, Yakobo akaenda Sukothi. Akajijengea makazi na pia vibanda vya mifugo yake. Hii ndiyo sababu mahali pale panaitwa Sukothi.
18 Baada ya Yakobo kutoka Padan-Aramu, alifika salama katika mji wa Shekemu huko Kanaani, na kuweka kambi yake karibu na mji huo.
19 Akanunua kiwanja kutoka kwa wana wa Hamori, baba wa Shekemu, kwa bei ya vipande mia moja vya fedha, akapiga hema lake hapo.
20 Akajenga madhabahu pale na kupaita El-Elohe-Israeli.