35
Furaha ya waliokombolewa
1 Jangwa na nchi kame vitafurahi;
nyika itashangilia na kuchanua maua.
Kama waridi,
2 litachanua maua,
litashangilia sana na kupaza sauti kwa furaha.
Litapewa utukufu wa Lebanoni,
fahari ya Karmeli na Sharoni;
wataona utukufu wa Mwenyezi Mungu,
fahari ya Mungu wetu.
3 Itieni nguvu mikono iliyo dhaifu,
yafanyeni imara magoti yaliyolegea,
4 waambieni wale wenye mioyo ya hofu,
“Kuweni hodari, msiogope;
tazama, Mungu wenu atakuja kulipa kisasi,
pamoja na ujira wake,
atakuja na kuwaokoa.”
5 Ndipo macho ya vipofu yatafumbuliwa
na masikio ya viziwi yatazibuliwa.
6 Ndipo kilema atarukaruka kama kulungu,
nao ulimi wa aliye bubu utapaza sauti kwa shangwe.
Maji yatatiririka kwa kasi katika nyika,
na vijito katika jangwa.
7 Mchanga wa moto utakuwa bwawa la maji,
ardhi yenye kiu itabubujika chemchemi.
Maskani ya mbweha walikolala hapo awali
patamea nyasi, matete na mafunjo.
8 Nako kutakuwa na njia kuu,
nayo itaitwa Njia ya Utakatifu.
Wasio safi hawatapita juu yake;
itakuwa ya wale wanaotembea katika Njia Ile;
yeye asafiriye juu yake,
ajapokuwa mjinga, hatapotea.
9 Huko hakutakuwa na simba,
wala mnyama mkali hatapita njia hiyo;
hawatapatikana humo.
Ila waliokombolewa tu ndio watakaopita huko,
10 waliokombolewa na Mwenyezi Mungu watarudi.
Wataingia Sayuni wakiimba;
furaha ya milele itakuwa juu ya vichwa vyao.
Watapata furaha na shangwe;
huzuni na majonzi vitakimbia.