11
Basi Yefta Mgileadi alikuwa shujaa mwenye nguvu. Baba yake alikuwa Gileadi, naye mama yake alikuwa kahaba. Mke wa Gileadi pia akamzalia wana, nao walipokua, wakamfukuza Yefta, na kumwambia, “Wewe huwezi kupata urithi katika jamii yetu, kwa sababu wewe ni mwana wa mwanamke mwingine.” Basi Yefta akawakimbia ndugu zake akaenda kuishi katika nchi ya Tobu, mahali ambako watu waasi walijiunga naye na kumfuata.
Baada ya muda Waamoni wakafanya vita na Israeli, viongozi wa Gileadi wakaenda kumchukua Yefta katika nchi ya Tobu. Wakamwambia Yefta, “Njoo, uwe jemadari wetu, ili tuweze kupigana na Waamoni.”
Yefta akawaambia viongozi wa Gileadi, “Je, si mlinichukia na kunifukuza nitoke katika nyumba ya baba yangu? Kwa nini mwanijia sasa, wakati mko taabuni?”
Viongozi wa Gileadi wakamwambia Yefta, “Lakini sasa tumegeuka kukuelekea wewe, ili uende pamoja nasi kupigana na Waamoni, nawe utakuwa kiongozi wetu juu ya watu wote wa Gileadi.”
Yefta akawaambia viongozi wa Gileadi, “Ikiwa mtanirudisha kwetu kupigana na Waamoni, naye Mwenyezi Mungu akanisaidia kuwashinda, je, ni kweli nitakuwa kiongozi wenu?”
10 Viongozi wa Gileadi wakamjibu Yefta, “Mwenyezi Mungu ndiye shahidi wetu. Kwa hakika tutafanya kama usemavyo.” 11 Basi Yefta akaenda na viongozi wa Gileadi, nao watu wakamfanya kiongozi na jemadari wao. Naye akarudia maneno yake yote mbele za Mwenyezi Mungu huko Mispa.
12 Ndipo Yefta akatuma wajumbe kwa mfalme wa Waamoni akisema, “Una nini nasi, hata umekuja kushambulia nchi yetu?”
13 Mfalme wa Waamoni akawajibu wajumbe wale wa Yefta, “Waisraeli walipopanda kutoka Misri, waliichukua nchi yangu kuanzia Mto Arnoni hadi Mto Yaboki, hadi kufikia Mto Yordani. Sasa irudishe kwa amani.”
14 Yefta akarudisha wajumbe kwa mfalme wa Waamoni, 15 kusema:
“Hili ndilo asemalo Yefta: Waisraeli hawakuchukua nchi ya Moabu wala nchi ya Waamoni. 16 Lakini walipopanda kutoka Misri, Waisraeli walipitia katika jangwa hadi Bahari ya Shamu na wakafika Kadeshi. 17 Ndipo Waisraeli wakatuma wajumbe kwa mfalme wa Edomu, wakisema, ‘Tupe ruhusa kupita katika nchi yako.’ Lakini mfalme wa Edomu hakutusikia. Wakatuma wajumbe pia kwa mfalme wa Moabu, naye akakataa. Kwa hiyo Waisraeli wakakaa huko Kadeshi.
18 “Baadaye wakasafiri kupitia jangwa, wakiambaa na nchi za Edomu na Moabu, wakapitia upande wa mashariki wa nchi ya Moabu, na kupiga kambi upande ule mwingine wa Mto Arnoni. Hawakuingia katika nchi ya Moabu, kwa kuwa Mto Arnoni ulikuwa mpaka wake.
19 “Kisha Waisraeli wakatuma wajumbe kwa Sihoni mfalme wa Waamori, aliyetawala Heshboni, na kumwambia, ‘Tupe ruhusa kupita katika nchi yako ili kufikia mahali petu.’ 20 Hata hivyo, Sihoni hakuwaamini Waisraeli kupita katika nchi yake. Akaandaa jeshi lake lote na kupiga kambi huko Yahasa, nao wakapigana na Waisraeli.
21 “Ndipo Mwenyezi Mungu, Mungu wa Israeli, akamtia Sihoni na watu wake wote mikononi mwa Waisraeli, nao wakawashinda. Waisraeli wakaimiliki nchi yote ya Waamori walioishi nchi hiyo, 22 wakiiteka nchi yote kuanzia Mto Arnoni hadi Mto Yaboki, na kutoka jangwani hadi Mto Yordani.
23 “Basi kwa kuwa Mwenyezi Mungu, Mungu wa Israeli, amewafukuza Waamori watoke mbele ya watu wake Israeli, wewe unayo haki gani ya kuitamalaki? 24 Je, haikupasi kuchukua kile ambacho mungu wako Kemoshi amekupa? Vivyo hivyo, chochote kile Mwenyezi Mungu, Mungu wetu, alichotupatia sisi, tutakimiliki. 25 Je, wewe ni bora kuliko Balaki mwana wa Sipori, mfalme wa Moabu? Je, yeye alishagombana na Waisraeli au kupigana nao wakati wowote? 26 Kwa maana kwa miaka mia tatu, Waisraeli wameishi Heshboni na makazi yake, Aroeri na makazi yake, na katika miji yote iliyo kando ya Mto Arnoni. Kwa nini wewe hukuyachukua wakati huo? 27 Mimi sijakukosea, bali wewe ndiwe unanikosea kwa kufanya vita nami. Basi Mwenyezi Mungu, aliye Mwamuzi, leo na aamue ugomvi kati ya Waisraeli na Waamoni.”
28 Hata hivyo, mfalme wa Waamoni hakuyajali maneno ya ujumbe wa Yefta.
29 Ndipo Roho wa Mwenyezi Mungu akaja juu ya Yefta. Akapita katikati ya Gileadi na Manase, pia akapita katika Mispa ya Gileadi, na kutokea huko akasonga mbele kushambulia Waamoni. 30 Naye Yefta akaweka nadhiri mbele za Mwenyezi Mungu akisema, “Ikiwa utawatia Waamoni mikononi mwangu, 31 chochote kile kitakachotoka katika mlango wa nyumba yangu cha kwanza ili kunilaki nirudipo kwa amani katika kuwashinda Waamoni, kitakuwa ni cha Mwenyezi Mungu na nitakitoa kuwa sadaka ya kuteketezwa.”
32 Ndipo Yefta akavuka kupigana na hao Waamoni, naye Mwenyezi Mungu akawatia mkononi mwake. 33 Akaharibu kabisa miji ishirini kuanzia Aroeri hadi karibu na Minithi, na kuendelea hadi Abel-Keramimu. Hivyo, Waisraeli wakawashinda Waamoni.
34 Yefta aliporudi nyumbani mwake huko Mispa, tazama, binti yake akatoka ili kumlaki kwa matari na kucheza. Alikuwa mwanawe wa pekee, hakuwa na mwana wala binti mwingine. 35 Alipomwona akararua mavazi yake akalia, “Ee! Binti yangu! Umenifanya niwe na huzuni na kunyong’onyea sana, kwa kuwa nimeweka nadhiri kwa Mwenyezi Mungu, ambayo siwezi kuivunja.”
36 Akajibu, “Baba yangu, umetoa neno lako kwa Mwenyezi Mungu. Nitendee mimi kama vile ulivyoahidi, kwa kuwa Mwenyezi Mungu amekupa ushindi dhidi ya adui zako Waamoni.” 37 Naye akamwambia baba yake, “Naomba nifanyiwe jambo hili. Nipewe miezi miwili ili kuzunguka vilimani nikaulilie ubikira wangu, mimi na wenzangu.”
38 Baba yake akamwambia, “Unaweza kwenda.” Naye akamwacha aende kwa miezi miwili. Hivyo akaondoka pamoja na wenzake, naye akaulilia ubikira wake huko vilimani kwa sababu hangeolewa kamwe. 39 Baada ya hiyo miezi miwili, alirejea kwa baba yake, naye baba yake akamtendea kama alivyokuwa ametoa nadhiri yake. Naye alikuwa bikira.
Nayo ikawa desturi katika Israeli, 40 kwamba kila mwaka binti za Israeli huenda kwa siku nne ili kumkumbuka huyo binti Yefta Mgileadi.