8
Ardhi ya Mshunami yarudishwa
Basi Al-Yasa alikuwa amemwambia yule mwanamke ambaye mwanawe alikuwa amefufuliwa, “Ondoka wewe na jamaa yako ukaishi mahali popote unapoweza kwa kitambo kidogo, kwa sababu Mwenyezi Mungu ameamuru njaa katika nchi hii ambayo itadumu kwa miaka saba.” Yule mwanamke akafanya kama vile yule mtu wa Mungu alivyosema. Yeye na jamaa yake wakaondoka na kwenda kuishi katika nchi ya Wafilisti kwa miaka saba.
Baada ya miaka saba, yule mwanamke akarudi kutoka nchi ya Wafilisti, akaenda kwa mfalme kumsihi kwa ajili ya nyumba yake na shamba lake. Mfalme alikuwa anazungumza na Gehazi, mtumishi wa mtu wa Mungu, naye alikuwa amesema, “Hebu niambie mambo yote makuu yaliyofanywa na Al-Yasa.” Gehazi alipokuwa akimweleza mfalme jinsi Al-Yasa alivyomfufua mtu, yule mwanamke ambaye mwanawe alikuwa amefufuliwa na Al-Yasa akaja ili amsihi mfalme kwa ajili ya nyumba yake na shamba lake.
Gehazi akasema, “Huyu ndiye huyo mwanamke, bwana wangu mfalme, na huyu ndiye mwanawe ambaye Al-Yasa alimfufua.” Mfalme akamuuliza yule mwanamke kuhusu mambo hayo, naye akamweleza.
Ndipo akaamuru afisa amshughulikie, kwa kumwambia, “Mrudishie huyu mwanamke kila kitu kilichokuwa mali yake, pamoja na mapato yote yaliyotokana na shamba lake tangu siku alipoondoka nchini hadi sasa.”
Hazaeli amuua Ben-Hadadi
Al-Yasa akaenda Dameski, naye Ben-Hadadi mfalme wa Aramu alikuwa mgonjwa. Mfalme alipoambiwa, “Mtu wa Mungu amekuja hadi hapa,” mfalme akamwambia Hazaeli, “Chukua zawadi na uende kumlaki mtu wa Mungu. Muulize Mwenyezi Mungu kupitia yeye, kwamba, ‘Je, nitapona ugonjwa huu?’ ”
Hazaeli akaenda kumlaki Al-Yasa, akiwa amechukua zawadi ya kila kitu kizuri kilichopatikana Dameski, mizigo iliyobebwa na ngamia arobaini. Akaingia ndani na kusimama mbele yake, akasema, “Mwanao Ben-Hadadi mfalme wa Aramu amenituma niulize, ‘Je, nitapona ugonjwa huu?’ ”
10 Al-Yasa akajibu, “Nenda ukamwambie, ‘Hakika utapona’; lakini Mwenyezi Mungu amenifunulia kwamba kweli atakufa.” 11 Al-Yasa akamkazia Hazaeli macho kwa nguvu hata akaona aibu. Kisha mtu wa Mungu akaanza kulia.
12 Hazaeli akauliza “Kwa nini bwana wangu analia?”
Al-Yasa akajibu, “Kwa sababu najua mabaya utakayowatendea Waisraeli. Utachoma moto ngome zao, utawaua vijana wao kwa upanga, kuwatupa chini kwa nguvu watoto wachanga, na kuwatumbua wanawake wenye mimba.”
13 Hazaeli akasema, “Itawezekanaje mtumishi wako, aliye mbwa tu, kufanya tendo la ajabu hivyo?”
Al-Yasa akamjibu, “Mwenyezi Mungu amenionesha kuwa utakuwa mfalme wa Aramu.”
14 Kisha Hazaeli akamwacha Al-Yasa na kumrudia bwana wake. Ben-Hadadi akamuuliza, “Al-Yasa alikuambia nini?” Hazaeli akajibu, “Aliniambia kwamba hakika utapona.” 15 Lakini kesho yake Hazaeli akachukua nguo nzito, akailoweka ndani ya maji, akaitandaza juu ya uso wa mfalme, hivyo akafa. Kisha Hazaeli akawa mfalme baada yake.
Yehoramu mfalme wa Yuda
(2 Nyakati 21:1-20)
16 Katika mwaka wa tano wa Yoramu mwana wa Ahabu mfalme wa Israeli, wakati huo Yehoshafati akiwa mfalme wa Yuda, Yehoramu mwana wa Yehoshafati akaanza kutawala kama mfalme wa Yuda. 17 Alikuwa na umri wa miaka thelathini na mbili alipoanza kutawala, naye akatawala huko Yerusalemu kwa miaka nane. 18 Akaenenda katika njia za wafalme wa Israeli, kama nyumba ya Ahabu ilivyokuwa imefanya, kwa kuwa alimwoa binti Ahabu. Akatenda maovu machoni pa Mwenyezi Mungu. 19 Hata hivyo, kwa ajili ya Daudi mtumishi wake, Mwenyezi Mungu hakutaka kuiangamiza Yuda. Alikuwa ameahidi kuidumisha taa kwa ajili ya Daudi na wazao wake milele.
20 Wakati wa utawala wa Yehoramu, Edomu waliasi dhidi ya Yuda na kujiwekea mfalme wao wenyewe. 21 Basi Yehoramu akaenda Sairi pamoja na magari yake yote ya vita. Waedomu wakamzunguka yeye na majemadari wake wa magari yake ya vita, lakini akaondoka, akapenya usiku na kuwashambulia Waedomu. Hata hivyo, jeshi lake likatorokea nyumbani mwao. 22 Hadi leo Edomu wameasi dhidi ya Yuda. Libna pia wakaasi wakati huo huo.
23 Kuhusu matukio mengine ya utawala wa Yehoramu na yote aliyoyafanya, je, hayakuandikwa katika kitabu cha kumbukumbu za wafalme wa Yuda? 24 Yehoramu akalala na baba zake, akazikwa pamoja nao katika Mji wa Daudi. Naye Ahazia mwanawe akawa mfalme baada yake.
Ahazia mfalme wa Yuda
(2 Nyakati 22:1-6)
25 Katika mwaka wa kumi na mbili wa utawala wa Yoramu mwana wa Ahabu mfalme wa Israeli, Ahazia mwana wa Yehoramu mfalme wa Yuda alianza kutawala. 26 Ahazia alikuwa na umri wa miaka ishirini na mbili alipoanza kutawala, naye akatawala katika Yerusalemu kwa mwaka mmoja. Mama yake aliitwa Athalia, mjukuu wa Omri mfalme wa Israeli. 27 Akaenenda katika njia za nyumba ya Ahabu, na kutenda maovu machoni pa Mwenyezi Mungu, kama nyumba ya Ahabu ilivyokuwa imefanya, kwa kuwa alikuwa ameoa kutoka nyumba ya Ahabu.
28 Ahazia akaenda vitani na Yoramu mwana wa Ahabu kupigana na Hazaeli mfalme wa Aramu huko Ramoth-Gileadi. Waaramu wakamjeruhi Yoramu. 29 Hivyo Mfalme Yoramu akarudi Yezreeli ili apate kuuguza majeraha aliyojeruhiwa na Waaramu huko Ramothi* alipopigana na Hazaeli mfalme wa Aramu.
Ndipo Ahazia mwana wa Yehoramu mfalme wa Yuda akashuka kwenda Yezreeli kumtazama Yoramu mwana wa Ahabu, kwa sababu alikuwa amejeruhiwa.
* 8:29 Rama kwa Kiebrania