Zaburi 142
Maombi ya kuokolewa dhidi ya watesi
Utenzi wa Daudi. Alipokuwa pangoni. Maombi.
1 Namlilia Mwenyezi Mungu kwa sauti,
napaza sauti yangu kwa Mwenyezi Mungu anihurumie.
2 Namimina malalamiko yangu mbele zake,
mbele zake naeleza shida zangu.
3 Roho yangu inapozimia ndani yangu,
wewe ndiwe unajua njia zangu.
Katika njia ninayopita,
watu wameniwekea mtego.
4 Tazama kuume kwangu na uone,
hakuna hata mmoja anayejihusisha nami.
Sina kimbilio,
hakuna anayejali maisha yangu.
5 Ee Mwenyezi Mungu, nakulilia wewe,
nasema, “Wewe ni kimbilio langu,
fungu langu katika nchi ya walio hai.”
6 Sikiliza kilio changu,
kwa sababu mimi ni mhitaji sana;
niokoe na wale wanaonifuatilia,
kwa kuwa wamenizidi nguvu.
7 Nifungue kutoka kifungo changu,
ili niweze kulisifu jina lako.
Ndipo wenye haki watanizunguka,
kwa sababu ya wema wako kwangu.