14
Mwenyezi Mungu yuaja kutawala
1 Siku ya Mwenyezi Mungu inakuja ambayo nyara zilizotekwa kwenu zitagawanywa miongoni mwenu.
2 Nitayakusanya mataifa yote huko Yerusalemu kupigana dhidi yake, mji utatekwa, nyumba zitavamiwa na kuporwa na wanawake watanajisiwa. Nusu ya mji wataenda uhamishoni, lakini watakaobaki hawataondolewa kutoka mjini.
3 Kisha Mwenyezi Mungu atatoka na kupigana dhidi ya watu wa yale mataifa, kama apiganavyo siku ya vita.
4 Siku hiyo miguu yake itasimama juu ya Mlima wa Mizeituni, mashariki mwa Yerusalemu, nao Mlima wa Mizeituni utagawanyika mara mbili kuanzia mashariki hadi magharibi, ukifanya bonde kubwa, nusu ya mlima ukisogea kuelekea kaskazini na nusu kuelekea kusini.
5 Nanyi mtakimbia kupitia katika bonde hilo la mlima wangu kwa kuwa litaenea hadi Aseli. Mtakimbia kama mlivyokimbia tetemeko la ardhi katika siku za Uzia mfalme wa Yuda. Kisha Mwenyezi Mungu, Mungu wangu, atakuja na watakatifu wote pamoja naye.
6 Siku hiyo hakutakuwa na nuru, baridi wala theluji.
7 Itakuwa siku ya kipekee, isiyo na mchana wala usiku, siku ijulikanayo na Mwenyezi Mungu. Jioni inapofika nuru itakuwepo.
8 Siku hiyo, maji yaliyo hai yatatiririka kutoka Yerusalemu, nusu kwenda kwenye bahari ya mashariki, na nusu kwenda kwenye bahari ya magharibi wakati wa kiangazi na wakati wa masika.
9 Mwenyezi Mungu atakuwa mfalme juu ya dunia yote. Katika siku hiyo atakuwa Mwenyezi Mungu mmoja, na jina lake litakuwa jina pekee.
10 Nchi yote kuanzia Geba, kaskazini mwa Yuda, hadi Rimoni, kusini mwa Yerusalemu, itakuwa kama Araba. Lakini Yerusalemu utainuliwa juu na kubaki mahali pake, toka Lango la Benyamini hadi mahali pa Lango la Kwanza, mpaka kwenye Lango la Pembeni na kutoka Mnara wa Hananeli hadi kwenye mashinikizo ya divai ya mfalme.
11 Utakaliwa na watu, kamwe hautaharibiwa tena, Yerusalemu utakaa salama.
12 Hii ndiyo tauni ambayo Mwenyezi Mungu atapiga nayo mataifa yote ambayo yalipigana dhidi ya Yerusalemu: Nyama ya miili yao itaoza wangali wamesimama kwa miguu yao, macho yao yataoza kwenye matundu yake na ndimi zao zitaoza vinywani mwao.
13 Katika siku hiyo Mwenyezi Mungu atawatia wanaume hofu kuu. Kila mwanaume atakamata mkono wa mwenzake nao watashambuliana.
14 Yuda pia atapigana katika Yerusalemu. Utajiri wa mataifa yote yanayoizunguka Yerusalemu utakusanywa, wingi wa dhahabu, fedha na mavazi.
15 Tauni ya aina hiyo hiyo itapiga farasi na nyumbu, ngamia na punda, nao wanyama wote walio kwenye kambi za adui.
16 Kisha walionusurika katika mataifa yote ambayo yaliushambulia Yerusalemu watakuwa wakipanda Yerusalemu kila mwaka kumwabudu Mfalme, Mwenyezi Mungu, Mungu wa majeshi ya mbinguni na kuadhimisha Sikukuu ya Vibanda.
17 Ikiwa taifa lolote la dunia hawataenda Yerusalemu kumwabudu Mfalme, Mwenyezi Mungu, Mungu wa majeshi ya mbinguni, mvua haitanyesha kwao.
18 Ikiwa watu wa Misri nao hawataenda kushiriki, hawatapata mvua. Mwenyezi Mungu ataleta juu yao tauni ambayo itayapiga mataifa ambayo hayataenda kuadhimisha Sikukuu ya Vibanda.
19 Hii itakuwa adhabu ya Misri na adhabu ya mataifa yote yale ambayo hayataenda Yerusalemu kuadhimisha Sikukuu ya Vibanda.
20 Katika siku hiyo, kengele zilizofungwa kwenye farasi zitaandikwa maneno haya: “Takatifu kwa Mwenyezi Mungu”. Navyo vyungu vya kupikia katika nyumba ya Mwenyezi Mungu vitakuwa kama bakuli takatifu mbele ya madhabahu.
21 Kila chungu kilicho Yerusalemu na Yuda kitakuwa kitakatifu kwa Mwenyezi Mungu, Mungu wa majeshi ya mbinguni, na wote wanaokuja kutoa dhabihu watachukua baadhi ya vyungu hivyo na kupikia. Katika siku hiyo hatakuwepo tena mfanyabiashara katika nyumba ya Mwenyezi Mungu, Mungu wa majeshi ya mbinguni.