2
Maandalizi Ya Kujenga Hekalu
(1 Wafalme 5:1-18)
Solomoni akatoa amri kujenga Hekalu kwa ajili ya Jina la Bwana na jumba la kifalme kwa ajili yake mwenyewe. Solomoni akaandika watu 70,000 kuwa wachukuzi wa mizigo, na watu 80,000 kuwa wachonga mawe vilimani, na watu 3,600 kuwa wasimamizi wao.
Solomoni akapeleka ujumbe huu kwa Mfalme Hiramu wa Tiro:
“Unitumie magogo ya mierezi kama ulivyomfanyia baba yangu Daudi wakati ulipompelekea mierezi ya kujenga jumba lake la kifalme la kuishi. Sasa ninakaribia kujenga Hekalu kwa ajili ya Jina la Bwana Mungu wangu na kuliweka wakfu kwake kwa ajili ya kufukizia uvumba wenye harufu nzuri mbele zake, mahali pa kuweka mikate ya Wonyesho kwa kufuata utaratibu na kwa ajili ya mahali pa kutolea sadaka za kuteketezwa kila siku asubuhi na jioni, siku za Sabato na Mwezi Mwandamo pia katika sikukuu zilizoamriwa za Bwana Mungu wetu. Hili ni agizo la kudumu kwa ajili ya Waisraeli.
“Hekalu nitakalolijenga litakuwa kubwa, kwa sababu Mungu wetu ni mkuu kuliko miungu mingine yote. Lakini ni nani awezaye kumjengea Hekalu, maadamu mbingu, hata mbingu zilizo juu sana, haziwezi kumtosha? Mimi ni nani basi hata nimjengee Hekalu, isipokuwa liwe tu mahali pa kutolea dhabihu za kuteketezwa mbele zake?
“Hivyo basi nitumie mtu mwenye ustadi wa kufanya kazi ya kutengeneza dhahabu na fedha, shaba na chuma, nyuzi za rangi ya zambarau, nyekundu na buluu, mwenye uzoefu wa kutia nakshi, ili afanye kazi Yuda na Yerusalemu pamoja na mafundi wangu wenye ustadi, ambao baba yangu Daudi aliwaweka.
“Pia nitumie magogo ya mierezi, miberoshi na misandali kutoka Lebanoni kwa maana najua kwamba watu wako wanao ujuzi wa kupasua mbao huko. Watu wangu watafanya kazi pamoja na watu wako ili wanipatie mbao kwa wingi kwa sababu Hekalu nitakalojenga lazima liwe kubwa na zuri kabisa. 10 Nitawapa watumishi wako, yaani, maseremala wakatao mbao, kori 20,000* Kori 20,000 za ngano ni sawa na lita 4,400. za unga wa ngano, kori 20,000 za shayiri, bathi 20,000 Bathi 20,000 za mvinyo au mafuta ni sawa na lita 440,000. za mvinyo, na bathi 20,000 za mafuta ya zeituni.”
11 Ndipo Hiramu mfalme wa Tiro akamjibu Solomoni kwa barua:
“Kwa sababu Bwana anawapenda watu wake, amekufanya wewe kuwa mfalme wao.”
12 Naye Hiramu akaongeza kusema:
“Ahimidiwe Bwana, Mungu wa Israeli aliyezifanya mbingu na nchi! Amempa Mfalme Daudi mwana mwenye hekima, aliyejaliwa maarifa na ufahamu, ambaye atajenga Hekalu kwa ajili ya Bwana, na jumba la kifalme kwa ajili yake mwenyewe.
13 “Mimi nitamtuma kwako Huramu-Abi, mtu mwenye ustadi mwingi, 14 ambaye mama yake alitoka Dani na baba yake alitoka Tiro. Yeye ni stadi wa kutengeneza vitu, kufanya kazi zote za dhahabu, fedha, shaba, chuma, mawe na mbao pamoja na kufuma. Ni stadi katika kutia rangi ya zambarau, buluu, nyekundu na nguo za kitani safi. Yeye ana ujuzi katika aina zote za kutia nakshi na anaweza kufuatiliza mchoro wowote wa kazi anayopewa. Atafanya kazi na mafundi wako na wale wa bwana wangu, Daudi baba yako.
15 “Sasa basi bwana wangu na awapelekee watumishi wake ngano, shayiri, mafuta ya zeituni na mvinyo kama alivyoahidi, 16 nasi tutakata magogo yote yale unayohitaji kutoka Lebanoni nasi tutayafunga pamoja na kuyaweka yaelee baharini mpaka Yafa. Kisha utaweza kuyachukua mpaka Yerusalemu.”
17 Ndipo Solomoni akaamuru ifanyike hesabu ya wageni wote waliokuwa katika Israeli, baada ya ile hesabu iliyofanywa na Daudi; wakapatikana watu 153,600. 18 Akawaweka watu 70,000 miongoni mwao kuwa wachukuzi wa mizigo, na 80,000 kuwa wachonga mawe vilimani, na 3,600 wakiwa wasimamizi juu yao ili wawahimize watu kufanya kazi.

*2:10 Kori 20,000 za ngano ni sawa na lita 4,400.

2:10 Bathi 20,000 za mvinyo au mafuta ni sawa na lita 440,000.