2
Hili ndilo asemalo Bwana:
“Kwa dhambi tatu za Moabu,
hata kwa dhambi nne, sitaizuia ghadhabu yangu.
Kwa sababu alichoma mifupa ya mfalme wa Edomu,
ikawa kama chokaa.
Nitatuma moto juu ya Moabu
ambao utateketeza ngome za Keriothi.
Moabu ataanguka kwa ghasia kubwa
katikati ya vilio vya vita na mlio wa tarumbeta.
Nitamwangamiza mtawala wake
na kuwaua maafisa wake wote pamoja naye,”
asema Bwana.
Hili ndilo asemalo Bwana:
“Kwa dhambi tatu za Yuda,
hata kwa dhambi nne, sitaizuia ghadhabu yangu.
Kwa sababu wameikataa sheria ya Bwana
na hawakuzishika amri zake,
kwa sababu wamepotoshwa na miungu ya uongo,
miungu ambayo babu zao waliifuata.
Nitatuma moto juu ya Yuda
ambao utateketeza ngome za Yerusalemu.”
Hukumu Juu Ya Israeli
Hili ndilo asemalo Bwana:
“Kwa dhambi tatu za Israeli,
hata kwa dhambi nne, sitaizuia ghadhabu yangu.
Wanawauza wenye haki kwa fedha,
na maskini kwa jozi ya viatu.
Wanakanyaga juu ya vichwa vya maskini,
kama vile juu ya mavumbi ya nchi,
na kukataa haki kwa walioonewa.
Baba na mwanawe hushiriki msichana mmoja,
kwa hivyo hulinajisi Jina langu takatifu.
Watu hulala kando ya kila madhabahu
juu ya nguo zilizowekwa rehani.
Katika nyumba ya mungu wao hunywa mvinyo
ulionunuliwa kwa fedha walizotozwa watu.
 
“Nilimwangamiza Mwamori mbele yao,
ingawa alikuwa mrefu kama mierezi,
na mwenye nguvu kama mialoni.
Niliyaangamiza matunda yake juu
na mizizi yake chini.
 
10 “Niliwapandisha toka Misri,
na nikawaongoza miaka arobaini jangwani
niwape nchi ya Waamori.
11 Pia niliinua manabii kutoka miongoni mwa wana wenu
na Wanadhiri kutoka miongoni mwa vijana wenu.
Je, hii si kweli, enyi watu wa Israeli?”
asema Bwana.
12 “Lakini mliwafanya Wanadhiri kunywa mvinyo
na kuwaamuru manabii wasitoe unabii.
 
13 “Sasa basi, nitawaponda
kama gari lipondavyo wakati limejazwa nafaka.
14 Mkimbiaji hodari hatanusurika,
wenye nguvu wataishiwa nguvu zao,
na shujaa hataweza kuokoa maisha yake.
15 Mpiga upinde atakimbia,
askari wapiga mbio hawataweza kutoroka,
na mpanda farasi hataokoa maisha yake.
16 Hata askari walio mashujaa sana
siku hiyo watakimbia uchi,”
asema Bwana.