2
Israeli Amwacha Mungu
Neno la Bwana lilinijia kusema, “Nenda ukahubiri masikioni mwa watu wa Yerusalemu:
“ ‘Nakumbuka moyo wako wa uchaji katika ujana wako,
jinsi ulivyonipenda kama bibi arusi
na kunifuata katika jangwa lile lote,
katika nchi isiyopandwa mbegu.
Israeli alikuwa mtakatifu kwa Bwana,
kama malimbuko ya kwanza ya mavuno yake;
wote waliowaangamiza walihesabiwa kuwa na hatia,
nayo maafa yaliwakumba,’ ”
asema Bwana.
 
Sikia neno la Bwana, ee nyumba ya Yakobo,
nanyi nyote jamaa za nyumba ya Israeli.
Hivi ndivyo asemavyo Bwana:
“Je, baba zenu waliona kosa gani kwangu,
hata wakatangatanga mbali nami hivyo?
Walifuata sanamu zisizofaa,
nao wenyewe wakawa hawafai.
Hawakuuliza, ‘Yuko wapi Bwana,
aliyetupandisha kutoka Misri
na kutuongoza kupitia nyika kame,
kupitia nchi ya majangwa na mabonde,
nchi ya ukame na giza,
nchi ambayo hakuna mtu asafiriye ndani yake
wala hakuna mtu aishiye humo?’
Niliwaleta katika nchi yenye wingi wa vitu
ili mpate kula matunda yake
na utajiri wa mazao yake.
Lakini mkaja na kuinajisi nchi yangu,
na kuufanya urithi wangu chukizo.
Makuhani hawakuuliza,
‘Yuko wapi Bwana?’
Wale wanaoshughulikia sheria hawakunijua mimi;
viongozi waliasi dhidi yangu.
Manabii walitabiri kwa jina la Baali,
wakifuata sanamu zisizofaa.
 
“Kwa hiyo naleta tena mashtaka dhidi yako,”
asema Bwana.
“Nami nitaleta mashtaka dhidi ya watoto wa watoto wako.
10 Vuka, nenda ngʼambo mpaka pwani ya Kitimu* Kitimu hapa ni Kipro, kisiwa katika Bahari ya Mediterania. nawe uangalie,
tuma watu waende Kedari, wachunguze kwa makini,
uone kama kumekuwepo kitu kama hiki.
11 Je, taifa limebadili miungu yake wakati wowote?
(Hata ingawa hao si miungu kamwe.)
Lakini watu wangu wamebadili Utukufu wao
kwa sanamu zisizofaa kitu.
12 Shangaeni katika hili, ee mbingu,
nanyi tetemekeni kwa hofu kuu,”
asema Bwana.
13 “Watu wangu wametenda dhambi mbili:
Wameniacha mimi,
niliye chemchemi ya maji yaliyo hai,
nao wamejichimbia visima vyao wenyewe,
visima vilivyobomoka, visivyoweza kuhifadhi maji.
14 Je, Israeli ni mtumishi, yaani mtumwa kwa kuzaliwa?
Kwa nini basi amekuwa mateka?
15 Simba wamenguruma;
wamemngurumia.
Wameifanya nchi yake kuwa ukiwa;
miji yake imeteketezwa, nayo imeachwa haina watu.
16 Pia watu wa Memfisi Memfisi kwa Kiebrania ni Nofu. na Tahpanhesi Tahpanhesi ni mji katika nchi ya Misri.
wamevunja taji ya kichwa chako.
17 Je, hukujiletea hili wewe mwenyewe
kwa kumwacha Bwana, Mungu wako
alipowaongoza njiani?
18 Sasa kwa nini uende Misri
kunywa maji ya Shihori?§ Kijito kinachoelekeza maji katika Mto Naili.
Nawe kwa nini kwenda Ashuru
kunywa maji ya Mto Frati?
19 Uovu wako utakuadhibu;
kurudi nyuma kwako kutakukemea.
Basi kumbuka, utambue
jinsi lilivyo ovu na chungu kwako
unapomwacha Bwana Mungu wako
na kutokuwa na hofu yangu,”
asema Bwana, Bwana Mwenye Nguvu Zote.
 
20 “Zamani nilivunja nira yako
na kukatilia mbali vifungo vyako;
ukasema, ‘Sitakutumikia!’
Naam kweli, kwenye kila kilima kirefu
na chini ya kila mti uliotanda matawi yake
ulijilaza kama kahaba.
21 Nilikupanda ukiwa mzabibu ulio bora sana,
mkamilifu na wa mbegu nzuri.
Ilikuwaje basi ukawa kinyume nami,
ukaharibika na kuwa mzabibu mwitu?
22 Hata ujisafishe kwa magadi
na kutumia sabuni nyingi,
bado doa la hatia yako liko mbele zangu,”
asema Bwana Mwenyezi.
23 “Wawezaje kusema, ‘Mimi si najisi,
sijawafuata Mabaali’?
Kumbuka jinsi ulivyotenda kule bondeni;
fikiri uliyoyafanya.
Wewe ni ngamia jike mwenye mbio
ukikimbia hapa na pale,
24 punda-mwitu aliyezoea jangwa,
anayenusa upepo katika tamaa yake kubwa:
katika wakati wake wa kuhitaji mbegu
ni nani awezaye kumzuia?
Madume yoyote yanayomfuatilia
hayana haja ya kujichosha;
wakati wa kupandwa kwake watampata tu.
25 Usikimbie hadi miguu yako iwe haina viatu,
na koo lako liwe limekauka.
Lakini ulisema, ‘Haina maana!
Ninaipenda miungu ya kigeni,
nami lazima niifuatie.’
 
26 “Kama vile mwizi aaibikavyo wakati amekamatwa,
hivyo ndivyo nyumba ya Israeli inavyoaibishwa:
wao wenyewe, wafalme wao na maafisa wao,
makuhani wao na manabii wao.
27 Wanaiambia miti, ‘Wewe ndiwe baba yangu,’
nalo jiwe, ‘Wewe ndiwe uliyenizaa.’
Wamenipa visogo vyao
wala hawakunigeuzia nyuso zao;
lakini wakiwa katika taabu, wanasema,
‘Njoo utuokoe!’
28 Iko wapi basi ile miungu mliyojitengenezea?
Yenyewe na ije kama inaweza kuwaokoa
wakati mko katika taabu!
Kwa maana mna miungu mingi
kama mlivyo na miji, ee Yuda.
 
29 “Kwa nini mnaleta mashtaka dhidi yangu?
Ninyi nyote mmeniasi,”
asema Bwana.
30 “Nimeadhibu watu wako bure tu,
hawakujirekebisha.
Upanga wako umewala manabii wako
kama simba mwenye njaa.
31 “Enyi wa kizazi hiki, tafakarini neno la Bwana:
“Je, nimekuwa jangwa kwa Israeli
au nchi ya giza kuu?
Kwa nini watu wangu wanasema, ‘Sisi tuko huru kuzurura,
hatutarudi kwako tena’?
32 Je, mwanamwali husahau vito vyake,
au bibi arusi mapambo yake ya arusi?
Lakini watu wangu wamenisahau mimi,
tena kwa siku zisizo na hesabu.
33 Je, wewe una ustadi kiasi gani katika kufuatia mapenzi!
Hata wale wanawake wabaya kuliko wote
wanaweza kujifunza kutokana na njia zako.
34 Katika nguo zako watu huona
damu ya uhai ya maskini wasio na hatia,
ingawa hukuwakamata wakivunja nyumba.
Lakini katika haya yote
35 unasema, ‘Sina hatia;
Mungu hajanikasirikia.’
Lakini nitakuhukumu kwa sababu unasema,
‘Mimi sijatenda dhambi.’
36 Kwa nini unatangatanga sana,
kubadili njia zako?
Utakatishwa tamaa na Misri
kama ulivyokatishwa na Ashuru.
37 Pia utaondoka mahali hapo
ukiwa umeweka mikono kichwani,
kwa kuwa Bwana amewakataa wale unaowatumainia;
hutasaidiwa nao.

*2:10 Kitimu hapa ni Kipro, kisiwa katika Bahari ya Mediterania.

2:16 Memfisi kwa Kiebrania ni Nofu.

2:16 Tahpanhesi ni mji katika nchi ya Misri.

§2:18 Kijito kinachoelekeza maji katika Mto Naili.