3
1 Vita kati ya nyumba ya Sauli na nyumba ya Daudi vilidumu kwa muda mrefu. Daudi akaendelea kuwa imara zaidi na zaidi, wakati nyumba ya Sauli iliendelea kudhoofika zaidi na zaidi.
2 Wana walizaliwa kwa Daudi huko Hebroni:
Mzaliwa wake wa kwanza alikuwa Amnoni mwana wa Ahinoamu wa Yezreeli;
3 mzaliwa wake wa pili alikuwa Danieli*au Kileabu mwana wa Abigaili, mjane wa Nabali wa Karmeli;
wa tatu, Absalomu mwana wa Maaka, binti Talmai mfalme wa Geshuri;
4 wa nne, Adoniya mwana wa Hagithi;
wa tano, Shefatia mwana wa Abitali;
5 wa sita, Ithreamu mwana wa Egla, mkewe Daudi.
Hawa ndio waliozaliwa kwa Daudi huko Hebroni.
Abneri amwendea Daudi
6 Wakati wa vita kati ya nyumba ya Sauli na nyumba ya Daudi, Abneri alikuwa anajiimarisha katika nafasi yake kwenye nyumba ya Sauli. 7 Basi Sauli alikuwa na suria, jina lake Rispa binti Aya. Naye Ish-Boshethi akamwambia Abneri, “Kwa nini umekutana kimwili na suria wa baba yangu?”
8 Abneri akakasirika sana kwa sababu ya kile Ish-Boshethi alichosema, naye akamjibu, “Je, mimi ni kichwa cha mbwa, kwa upande wa Yuda? Siku hii ya leo mimi ni mtiifu kwa nyumba ya baba yako Sauli, kwa jamaa yake na rafiki zake. Sijakukabidhi kwa Daudi, lakini bado unanilaumu kwa kosa la kuhusika na huyu mwanamke! 9 Mungu na amwadhibu Abneri vikali zaidi ikiwa sitafanya kwa ajili ya Daudi kile Mwenyezi Mungu alichomwahidi kwa kiapo, 10 na kuuhamisha ufalme kutoka nyumba ya Sauli na kuimarisha kiti cha ufalme cha Daudi juu ya Israeli na Yuda kuanzia Dani hadi Beer-Sheba.” 11 Ish-Boshethi hakuthubutu kusema neno jingine kwa Abneri, kwa sababu alimwogopa Abneri.
12 Ndipo Abneri akatuma wajumbe kwa niaba yake kwa Daudi, kumwambia, “Nchi hii ni ya nani? Fanya mapatano na mimi, nami nitakusaidia kuiweka Israeli yote juu yako.”
13 Daudi akasema, “Vyema, nitafanya mapatano nawe. Lakini nahitaji jambo moja kwako: Usije mbele yangu hadi umemleta Mikali binti Sauli wakati utakapokuja kuniona.” 14 Kisha Daudi akapeleka wajumbe kwa Ish-Boshethi mwana wa Sauli, kudai, “Nipe Mikali mke wangu, ambaye nilimposa mwenyewe kwa mahari ya magovi mia moja ya Wafilisti.”
15 Kwa hiyo Ish-Boshethi akatoa amri kwamba Mikali achukuliwe kutoka kwa Paltieli mumewe, mwana wa Laishi. 16 Hata hivyo, mumewe alienda pamoja naye, akilia nyuma ya mkewe njia yote hadi Bahurimu. Ndipo Abneri akamwambia Paltieli, “Rudi nyumbani!” Kwa hiyo akarudi.
17 Abneri akafanya shauri pamoja na wazee wa Israeli, akasema, “Muda mrefu mmetaka kumfanya Daudi mfalme wenu. 18 Sasa fanyeni hivyo! Kwa maana Mwenyezi Mungu alimwahidi Daudi akisema, ‘Kupitia Daudi mtumishi wangu nitawaokoa watu wangu Israeli kutoka mikononi mwa Wafilisti na kutoka mikononi mwa adui zako wote.’ ”
19 Pia Abneri mwenyewe akazungumza na kabila la Benyamini. Kisha akaenda Hebroni kumwambia Daudi kila kitu ambacho Israeli na nyumba yote ya Benyamini walichotaka kufanya. 20 Abneri, aliyekuwa na watu ishirini pamoja naye, alipokuja kwa Daudi huko Hebroni, Daudi akamwandalia karamu pamoja na watu wake. 21 Ndipo Abneri akamwambia Daudi, “Niache niende mara moja nikakusanye Israeli yote kwa ajili ya mfalme bwana wangu, ili waweze kufanya mapatano na wewe, ili uweze kutawala yale yote moyo wako unaonea shauku.” Basi Daudi akamuaga Abneri, naye akaenda kwa amani.
Yoabu amuua Abneri
22 Wakati huo huo, watu wa Daudi na Yoabu walirudi kutoka kushambulia, nao wakarudi na nyara nyingi mno. Lakini Abneri hakuwa tena pamoja na Daudi huko Hebroni, kwa sababu Daudi alikuwa amemruhusu aende zake, naye akaenda kwa amani. 23 Yoabu na askari wote aliokuwa nao walipowasili, aliambiwa kwamba Abneri mwana wa Neri alikuwa amekuja kwa mfalme, na kwamba mfalme alikuwa amemruhusu aende zake, na kwamba alikuwa ameondoka kwa amani.
24 Basi Yoabu alienda kwa mfalme na kumwambia, “Ni nini hiki ulichofanya? Tazama, Abneri alikuja kwako. Kwa nini ukamwacha aende? Sasa ameenda! 25 Unajua Abneri mwana wa Neri alikuja kukudanganya na kuchunguza mienendo yako, na kugundua kila kitu unachokifanya.”
26 Ndipo Yoabu akamwacha Daudi na kutuma wajumbe wamfuate Abneri, nao wakamrudisha kutoka kisima cha Sira. Lakini Daudi hakufahamu jambo hili. 27 Basi Abneri aliporudi Hebroni, Yoabu akamchukua kando ndani ya lango, kama vile kuzungumza naye faraghani. Ili kulipiza kisasi damu ya nduguye Asaheli, Yoabu akamchoma mkuki tumboni palepale, naye akafa.
28 Baadaye, Daudi aliposikia kuhusu jambo hili, akasema, “Mimi na ufalme wangu kamwe hatuna hatia mbele za Mwenyezi Mungu kuhusu damu ya Abneri mwana wa Neri. 29 Damu yake na iwe juu ya kichwa cha Yoabu na juu ya nyumba yote ya baba yake! Kamwe asikosekane yeyote katika nyumba ya Yoabu mwenye kidonda chenye usaha au ukoma, au mwenye kuegemea fimbo, au aangukaye kwa upanga, au kupungukiwa na chakula.”
30 (Yoabu na Abishai ndugu yake walimuua Abneri kwa sababu alikuwa amemuua Asaheli ndugu yao katika vita huko Gibeoni.)
31 Kisha Daudi akamwambia Yoabu na watu wote aliokuwa pamoja nao, “Rarueni nguo zenu na mvae gunia, mtembee mkiomboleza mbele ya Abneri.” Mfalme Daudi mwenyewe akatembea nyuma ya jeneza. 32 Wakamzika Abneri huko Hebroni, naye mfalme akalia kwa sauti kwenye kaburi la Abneri. Pia watu wote wakalia.
33 Mfalme akaimba ombolezo hili kwa ajili ya Abneri:
“Je, ilipasa Abneri afe kama anavyokufa mpumbavu?
34 Mikono yako haikufungwa,
miguu yako haikufungwa pingu.
Ulianguka kama yeye aangukaye
mbele ya watu waovu.”
Nao watu wote wakamlilia tena.
35 Kisha watu wote wakaja kumsihi Daudi ale chochote kulipokuwa bado mchana; lakini Daudi akaapa, akisema, “Mungu na aniadhibu vikali zaidi, nikionja mkate au kitu kingine chochote kabla ya jua kutua!”
36 Watu wote wakaona hilo nao ikawapendeza; naam, kila kitu mfalme alichofanya kiliwapendeza. 37 Kwa hiyo siku ile watu wote na Israeli yote wakajua kwamba mfalme hakushiriki katika mauaji ya Abneri mwana wa Neri.
38 Kisha mfalme akawaambia watu wake, “Je, hamfahamu kwamba mtu mkuu na mashuhuri ameanguka katika Israeli leo? 39 Nami leo ingawa ni mfalme mpakwa mafuta, mimi ni dhaifu, nao hawa wana wa Seruya wananizidi nguvu. Mwenyezi Mungu na amlipize mtenda maovu sawasawa na matendo yake maovu!”