12
Yakobo auawa, Petro atiwa gerezani
Wakati huo huo Mfalme Herode Agripa aliwakamata baadhi ya waumini wa Isa. Akaamuru Yakobo, ndugu yake Yohana, auawe kwa upanga. Alipoona jambo hilo limewapendeza Wayahudi, akaendelea, akamkamata Petro pia. Hii ilitokea wakati wa Sikukuu ya Mikate Isiyotiwa Chachu. Baada ya kumkamata alimfunga gerezani chini ya ulinzi wa vikundi vinne vya askari, vyenye askari wanne kila kimoja. Herode alikuwa amekusudia kumfanyia mashtaka mbele ya watu baada ya Pasaka*Sherehe iliyowakumbusha Waisraeli jinsi Mwenyezi Mungu alivyowakomboa kutoka utumwani huko Misri..
Kwa hiyo Petro akawekwa gerezani, lakini waumini wa Isa walikuwa wakimwombea kwa Mungu kwa bidii.
Usiku ule kabla ya siku ambayo Herode Agripa alikuwa amekusudia kumfanyia mashtaka, Petro alikuwa amelala kati ya askari wawili, akiwa amefungwa kwa minyororo miwili. Nao walinzi wa zamu walikuwa wakilinda lango la gereza. Ghafula malaika wa Mwenyezi Mungu akatokea, na nuru ikamulika mle ndani ya gereza. Yule malaika akampiga Petro ubavuni na kumwamsha, akisema, “Ondoka upesi!” Mara ile minyororo ikaanguka kutoka mikononi mwa Petro.
Yule malaika akamwambia, “Vaa nguo zako na viatu vyako.” Petro akafanya hivyo. Kisha akamwambia, “Jifunge vazi lako na unifuate.” Petro akatoka mle gerezani akiwa amefuatana na yule malaika. Hakujua wakati huo kuwa yaliyokuwa yakitukia yalikuwa kweli. Alidhani kuwa anaona maono. 10 Walipita kundi la kwanza la walinzi na la pili, wakafika kwenye lango la chuma linaloelekea mjini. Lango likawafungukia lenyewe, nao wakapita hapo, wakatoka nje. Baada ya kutembea umbali wa mtaa mmoja, ghafula yule malaika akamwacha Petro.
11 Ndipo Petro akarudiwa na fahamu, akasema, “Sasa ninajua bila shaka yoyote kuwa Mwenyezi Mungu amemtuma malaika wake na kuniokoa kutoka makucha ya Herode Agripa na kutoka matazamio yote ya Wayahudi.”
12 Mara Petro alipotambua hili alienda nyumbani mwa Mariamu, mama yake Yohana aliyeitwa pia Marko, ambako watu wengi walikuwa wamekutana kwa maombi. 13 Petro alipobisha hodi kwenye lango la nje, mjakazi aliyeitwa Roda akaja kumfungulia. 14 Alipoitambua sauti ya Petro, alifurahi mno akarudi bila kufungua lango, akapaza sauti, akasema, “Petro yuko langoni!”
15 Wakamwambia yule mjakazi, “Umerukwa na akili.” Alipozidi kusisitiza kuwa ni kweli, wakasema, “Lazima awe ni malaika wake.”
16 Lakini Petro aliendelea kugonga langoni, nao walipofungua lango na kumwona Petro, walistaajabu sana. 17 Yeye akawaashiria kwa mkono wake wanyamaze kimya, akawaeleza jinsi Mwenyezi Mungu alivyomtoa gerezani. Naye akaongeza kusema, “Waelezeni Yakobo na ndugu wengine habari hizi.” Kisha akaondoka akaenda sehemu nyingine.
18 Kulipokucha kukawa na fadhaa kubwa miongoni mwa wale askari kuhusu yaliyomtukia Petro. 19 Baada ya Herode kuamuru atafutwe kila mahali na bila kumpata, aliwahoji wale askari walinzi kisha akatoa amri wauawe. Basi Herode Agripa akatoka Yudea akaenda Kaisaria, akakaa huko kwa muda.
Kifo cha Herode Agripa
20 Basi Herode Agripa alikuwa amekasirishwa sana na watu wa Tiro na Sidoni. Hivyo watu wa miji hiyo miwili wakaungana pamoja wakataka kukutana naye. Baada ya kuungwa mkono na Blasto, mtumishi maalum wa Mfalme Herode Agripa aliyeaminika, wakaomba mapatano ya amani maana nchi zao zilitegemea nchi ya huyo mfalme kwa mahitaji yao ya chakula.
21 Katika siku iliyochaguliwa Herode Agripa akavaa mavazi yake ya kifalme, akaketi kwenye kiti chake cha utawala, akawahutubia watu. 22 Watu waliokuwa wamekusanyika wakapaza sauti, wakisema, “Hii si sauti ya mwanadamu, bali ni ya Mungu!” 23 Ghafula, kwa kuwa Herode hakumpa Mungu utukufu, malaika wa Mwenyezi Mungu akampiga, naye akaliwa na chango, akafa.
24 Lakini neno la Mungu likaendelea mbele na kuenea, nao wengi wakaambatana nalo.
25 Barnaba na Sauli walipomaliza ile huduma yao iliyowapeleka, wakarudi Yerusalemu wakiwa pamoja na Yohana aitwaye Marko.

*12:4 Sherehe iliyowakumbusha Waisraeli jinsi Mwenyezi Mungu alivyowakomboa kutoka utumwani huko Misri.