3
Kuanguka kwa mwanadamu
Basi nyoka alikuwa mjanja kuliko wanyama pori wote ambao Bwana Mwenyezi Mungu aliwafanya. Nyoka akamwambia mwanamke, “Ati Mungu alisema, ‘Kamwe msile matunda ya mti wowote wa bustanini’?”
Mwanamke akamjibu nyoka, “Tunaweza kula matunda ya miti iliyo katika bustani, lakini Mungu alisema, ‘Kamwe msile tunda la mti ulio katikati ya bustani, wala kuugusa, la sivyo mtakufa.’ ”
Lakini nyoka akamwambia mwanamke, “Hakika hamtakufa. Kwa maana Mungu anajua kwamba mtakapokula tunda hilo, macho yenu yatafumbuliwa, nanyi mtakuwa kama Mungu, mkijua mema na mabaya.”
Mwanamke alipotambua kwamba tunda la mti huo lilikuwa zuri kwa chakula na la kupendeza macho, tena linatamanika kwa kujipatia hekima, basi akachuma matunda yake, akala. Pia akampa mumewe, aliyekuwa pamoja naye, akala. Ndipo macho yao wote wawili yakafumbuliwa, wakajiona kwamba walikuwa uchi; hivyo wakashona majani ya mtini, wakajifunika.
Yule mwanaume na mkewe waliposikia sauti ya Bwana Mwenyezi Mungu akitembea bustanini jioni, wakajificha kutoka kwa Bwana Mwenyezi Mungu katikati ya miti ya bustani. Lakini Bwana Mwenyezi Mungu akamwita Adamu, “Uko wapi?”
10 Naye akajibu, “Nilikusikia katika bustani nikaogopa kwa sababu nilikuwa uchi, hivyo nikajificha.”
11 Mungu akamuuliza, “Ni nani aliyekuambia ya kuwa ulikuwa uchi? Je, umekula matunda ya mti niliokuamuru usile?”
12 Adamu akasema, “Huyu mwanamke uliyenipa awe pamoja nami alinipa matunda ya huo mti, nami nikala.”
13 Ndipo Bwana Mwenyezi Mungu akamuuliza mwanamke, “Umefanya jambo gani?” Mwanamke akajibu, “Nyoka alinidanganya, nami nikala.”
14 Hivyo Bwana Mwenyezi Mungu akamwambia nyoka, “Kwa kuwa umefanya hili,
“Umelaaniwa kuliko mifugo wote
na wanyama pori wote!
Utatambaa kwa tumbo lako
na kula mavumbi
siku zote za maisha yako.
15 Nami nitaweka uadui
kati yako na huyu mwanamke,
na kati ya uzao wako na wake;
yeye atakuponda kichwa,
nawe utamuuma kisigino.”
16 Kwa mwanamke akasema,
“Nitakuzidishia sana uchungu wakati wa kuzaa kwako;
kwa uchungu utazaa watoto.
Tamaa yako itakuwa kwa mumeo,
naye atakutawala.”
17 Akamwambia Adamu, “Kwa sababu umemsikiliza mke wako na ukala kutoka mti niliokuamuru, ‘Msile tunda lake,’
“Ardhi imelaaniwa kwa sababu yako;
kwa kazi ngumu utakula chakula kitokacho humo
siku zote za maisha yako.
18 Itakuzalia miiba na mibaruti,
nawe utakula mimea ya shambani.
19 Kwa jasho la uso wako
utakula chakula chako
hadi utakaporudi ardhini,
kwa kuwa ulitwaliwa kutoka humo;
wewe u mavumbi
na mavumbini utarudi.”
20 Adamu akamwita mkewe jina Hawa, kwa kuwa atakuwa mama wa wote walio hai.
21 Bwana Mwenyezi Mungu akawatengenezea Adamu na mkewe mavazi ya ngozi, akawavika. 22 Kisha Bwana Mwenyezi Mungu akasema, “Sasa mtu huyu amekuwa kama mmoja wetu, kwa kujua mema na mabaya. Sharti asiruhusiwe kunyoosha mkono wake na kuchuma pia kutoka mti wa uzima akala, naye akaishi milele.” 23 Hivyo Bwana Mwenyezi Mungu akamfukuzia mbali kutoka Bustani ya Edeni, akalime ardhi ambamo alitolewa. 24 Baada ya kumfukuzia mbali Adamu, Mungu akaweka makerubi mashariki mwa Bustani ya Edeni, pamoja na upanga wa moto ukimulika kila upande kulinda njia ya kuuendea mti wa uzima.