11
Mnara wa Babeli
1 Wakati huo dunia yote ilikuwa na lugha moja na msemo mmoja. 2 Watu walipoelekea upande wa mashariki, wakafika kwenye tambarare katika nchi ya Shinari*yaani Babeli, nao wakaishi huko.
3 Wakasemezana wao kwa wao, “Njooni, tufyatue matofali na tuyachome vizuri kwa moto.” Walitumia matofali badala ya mawe, na lami kuunganisha hayo matofali. 4 Ndipo wakasema, “Njooni, tujijengee mji wenye mnara ambao utafika hadi mbinguni, ili tujipatie jina, tusije tukatawanyika duniani kote.”
5 Lakini Mwenyezi Mungu akashuka ili auone mji na mnara ambao wanadamu walikuwa wanaujenga. 6 Mwenyezi Mungu akasema, “Ikiwa kama taifa moja wanaozungumza lugha moja wameanza kufanya hili, basi hakuna lolote watakalopanga kufanya ambalo halitawezekana kwao. 7 Njooni, tushuke tuvuruge lugha yao ili wasielewane wao kwa wao.”
8 Hivyo Mwenyezi Mungu akawatawanya kutoka mahali pale waende duniani kote; nao wakaacha kuujenga huo mji. 9 Ndiyo maana pakaitwa Babeli, kwa sababu hapo ndipo Mwenyezi Mungu alipoivuruga lugha ya dunia nzima. Kutoka hapo Mwenyezi Mungu akawatawanya duniani kote.
Vizazi vya Shemu hadi Abramu
(1 Nyakati 1:24-27)
10 Hivi ndivyo vizazi vya Shemu.
Miaka miwili baada ya gharika, Shemu alipokuwa na umri wa miaka mia moja, akamzaa Arfaksadi. 11 Baada ya kumzaa Arfaksadi, Shemu aliishi miaka mia tano, akazaa watoto wengine wa kiume na wa kike.
12 Arfaksadi alipokuwa ameishi miaka thelathini na tano, akamzaa Shela. 13 Baada ya kumzaa Shela, Arfaksadi aliishi miaka mia nne na tatu (403), akazaa watoto wengine wa kiume na wa kike.
14 Shela alipokuwa ameishi miaka thelathini, akamzaa Eberi. 15 Baada ya kumzaa Eberi, Shela aliishi miaka mia nne na tatu (403), akazaa watoto wengine wa kiume na wa kike.
16 Eberi alipokuwa ameishi miaka thelathini na nne, akamzaa Pelegi. 17 Baada ya kumzaa Pelegi, Eberi aliishi miaka mia nne na thelathini (430), akazaa watoto wengine wa kiume na wa kike.
18 Pelegi alipokuwa ameishi miaka thelathini, akamzaa Reu. 19 Baada ya kumzaa Reu, Pelegi aliishi miaka mia mbili na tisa (209), akazaa watoto wengine wa kiume na wa kike.
20 Reu alipokuwa ameishi miaka thelathini na mbili, akamzaa Serugi. 21 Baada ya kumzaa Serugi, Reu aliishi miaka mia mbili na saba (207), akazaa watoto wengine wa kiume na wa kike.
22 Serugi alipokuwa ameishi miaka thelathini, akamzaa Nahori. 23 Baada ya kumzaa Nahori, Serugi aliishi miaka mia mbili, akazaa watoto wengine wa kiume na wa kike.
24 Nahori alipokuwa ameishi miaka ishirini na tisa, akamzaa Tera. 25 Baada ya kumzaa Tera, Nahori aliishi miaka mia moja na kumi na tisa (119), akazaa watoto wengine wa kiume na wa kike.
26 Tera alipokuwa ameishi miaka sabini, akamzaa Abramu, na baadaye akawazaa Nahori na Harani.
Wazao wa Tera
27 Hivi ndivyo vizazi vya Tera.
Tera aliwazaa Abramu, Nahori na Harani. Harani akamzaa Lutu. 28 Tera alipokuwa bado hai, Harani akafa katika Uru ya Wakaldayo, nchi aliyozaliwa. 29 Abramu na Nahori walioa. Mke wa Abramu aliitwa Sarai, naye mke wa Nahori aliitwa Milka; Milka na Iska walikuwa watoto wa Harani. 30 Sarai alikuwa tasa, hakuwa na watoto.
31 Tera akawachukua Abramu mwanawe, mjukuu wake Lutu mwana wa Harani, na Sarai mkwewe, mke wa Abramu mwanawe, wakatoka Uru ya Wakaldayo pamoja, wakaenda nchi ya Kanaani. Lakini walipofika Harani, wakaishi huko.
32 Tera aliishi miaka mia mbili na mitano (205), akafa huko Harani.