42
Ndugu za Yusufu waenda Misri
1 Yakobo alipofahamu kuwa kuna nafaka kule Misri, akawaambia wanawe, “Mbona mnakaa tu hapa mkitazamana?” 2 Akaendelea kuwaambia, “Nimesikia kuwa huko Misri kuna nafaka. Teremkeni huko mkatununulie chakula, ili tuweze kuishi wala tusife.”
3 Ndipo ndugu kumi wa Yusufu wakateremka huko Misri kununua nafaka. 4 Lakini Yakobo hakumtuma Benyamini, ndugu yake Yusufu, pamoja na wengine, kwa sababu aliogopa asije akapatwa na madhara. 5 Hivyo wana wa Israeli walikuwa miongoni mwa wale walioenda Misri kununua nafaka, kwani njaa ilikuwa katika nchi ya Kanaani pia.
6 Wakati huo Yusufu alikuwa mtawala wa nchi ya Misri, na ndiye aliwauzia watu wote nafaka. Kwa hiyo wakati ndugu zake Yusufu walifika, wakamsujudia hadi nyuso zao zikagusa ardhi. 7 Mara Yusufu alipowaona ndugu zake, akawatambua. Lakini akajifanya mgeni na kuzungumza nao kwa ukali, akiwauliza, “Ninyi mnatoka wapi?”
Wakamjibu, “Tumetoka nchi ya Kanaani kuja kununua chakula.”
8 Ingawa Yusufu aliwatambua ndugu zake, wao hawakumtambua. 9 Ndipo Yusufu alipokumbuka ndoto zake kuwahusu, akawaambia, “Ninyi ni wapelelezi! Mmekuja kuangalia mahali nchi yetu haina ulinzi.”
10 Wakamjibu, “Sivyo, bwana. Watumishi wako wamekuja kununua chakula. 11 Sisi sote ni wana wa baba mmoja. Watumishi wako ni watu waaminifu, wala sio wapelelezi.”
12 Akawaambia, “La, hasha! Mmekuja kuangalia mahali nchi yetu haina ulinzi.”
13 Lakini wakamjibu, “Watumishi wako walikuwa ndugu kumi na wawili, wana wa mtu mmoja ambaye anaishi katika nchi ya Kanaani. Sasa mdogo wetu wa mwisho yupo na baba yetu, na mwingine alikufa.”
14 Yusufu akawaambia, “Kama nilivyowaambia: Ninyi ni wapelelezi! 15 Hivi ndivyo mtakavyojaribiwa: Hakika kama Farao aishivyo, hamtaondoka mahali hapa hadi ndugu yenu mdogo aje hapa. 16 Tumeni mmoja wenu akamlete huyo ndugu yenu. Wengine mtawekwa gerezani, ili maneno yenu yajaribiwe kuona kama mnasema kweli. La sivyo, hakika kama Farao aishivyo ninyi ni wapelelezi!” 17 Akawaweka wote chini ya ulinzi kwa siku tatu.
18 Siku ya tatu, Yusufu akawaambia, “Fanyeni hili nanyi mtaishi, kwa maana namwogopa Mungu: 19 Ikiwa ninyi ni watu waaminifu, mmoja wa ndugu zenu na abaki kifungoni, nanyi wengine pelekeni nafaka kwa jamaa yenu wanaoteseka kwa njaa. 20 Lakini lazima mniletee ndugu yenu mdogo hapa, ili maneno yenu yathibitike na kwamba msife.” Wakakubali kufanya hivyo.
21 Wakaambiana wao kwa wao, “Hakika tunaadhibiwa kwa sababu ya ndugu yetu. Tuliona jinsi alivyohuzunika alipokuwa anatusihi kuokoa maisha yake, lakini hatukumsikiliza. Hiyo ndiyo sababu dhiki hii imetupata.”
22 Reubeni akawajibu, “Sikuwaambieni msitende dhambi dhidi ya kijana? Lakini hamkunisikiliza! Sasa ni lazima tuadhibiwe kwa ajili ya damu yake.” 23 Hawakujua kuwa Yusufu angewaelewa, kwa sababu alitumia mkalimani.
24 Yusufu akajitenga nao, akaanza kulia, kisha akawarudia na kuzungumza nao tena. Akaamuru Simeoni akamatwe na kufungwa mbele yao.
25 Yusufu akatoa amri ya kujaza magunia yao nafaka na kuweka fedha ya kila mmoja ndani ya gunia lake, kisha wapewe chakula cha njiani. Baada ya kutendewa hayo yote, 26 wakapakiza nafaka juu ya punda wao, wakaondoka.
27 Walipofika mahali pa kulala huko njiani, mmoja wao akafungua gunia lake ili amlishe punda wake; akakuta fedha yake ndani ya gunia lake. 28 Akawaambia ndugu zake, “Fedha yangu imerudishwa. Iko ndani ya gunia langu.”
Mioyo yao ikazimia, na kila mmoja akamgeukia mwenzake wakitetemeka, wakaulizana, “Ni nini hiki Mungu alichotufanyia?”
29 Walipofika kwa Yakobo baba yao katika nchi ya Kanaani, wakamweleza mambo yote yaliyowapata. Wakasema, 30 “Huyo mtu aliye bwana katika nchi hiyo alisema nasi kwa ukali, akatutendea kana kwamba sisi tulikuwa tunaipeleleza nchi. 31 Lakini tulimwambia, ‘Sisi ni watu waaminifu, sio wapelelezi. 32 Tulizaliwa ndugu kumi na wawili, wana wa baba mmoja. Mmoja alikufa, na mdogo wetu wa mwisho yupo na baba yetu huko Kanaani.’
33 “Ndipo huyo mtu aliye bwana katika nchi hiyo alipotuambia, ‘Hivi ndivyo nitafahamu kuwa ninyi ni watu waaminifu: Mwacheni mmoja wa ndugu zenu hapa kwangu, kisha nendeni mpeleke chakula kwa jamaa yenu inayoteseka kwa njaa. 34 Lakini mleteni huyo ndugu yenu mdogo kwangu. Ndipo nitajua kuwa ninyi sio wapelelezi, ila ni watu waaminifu. Kisha nitamrudisha ndugu yenu, nanyi mtaweza kufanya biashara katika nchi hii.’ ”
35 Walipokuwa wanamimina nafaka kutoka magunia yao, tazama! Wakapata ndani ya gunia la kila mtu mfuko wa fedha. Wakati wao na baba yao waliona mifuko ya fedha, wakaogopa. 36 Yakobo baba yao akawaambia, “Ninyi mmenipokonya watoto wangu. Yusufu hayupo na Simeoni hayupo; tena na sasa mnataka kumchukua Benyamini. Kila kitu ni kinyume nami!”
37 Ndipo Reubeni akamwambia baba yake, “Unaweza kuwaua wanangu wote wawili, ikiwa sitamrudisha Benyamini kwako. Mkabidhi Benyamini katika uangalizi wangu, nami nitamrudisha.”
38 Lakini Yakobo akasema, “Mwanangu hatashuka huko pamoja nanyi; ndugu yake amekufa, naye ndiye peke yake aliyebaki. Akipatwa na madhara katika safari mnayoiendea, mtashusha kichwa changu chenye mvi kaburini kwa masikitiko.”