12
Kushukuru na kusifu 
  1 Katika siku ile utasema:  
“Nitakusifu wewe, Ee Mwenyezi Mungu.  
Ingawa ulinikasirikia,  
hasira yako imegeukia mbali  
nawe umenifariji.   
 2 Hakika Mungu ni wokovu wangu;  
nitamtumaini wala sitaogopa.  
Mwenyezi Mungu, Mwenyezi Mungu,  
ni nguvu zangu na wimbo wangu;  
amekuwa wokovu wangu.”   
 3 Kwa furaha mtachota maji  
kutoka visima vya wokovu.   
 4 Katika siku hiyo mtasema:  
“Mshukuruni Mwenyezi Mungu, mliitie jina lake;  
julisheni miongoni mwa mataifa yale aliyoyafanya,  
tangazeni kuwa jina lake limetukuka.   
 5 Mwimbieni Mwenyezi Mungu, kwa kuwa ametenda mambo makuu,  
hili na lijulikane duniani kote.   
 6 Pazeni sauti mwimbe kwa furaha, watu wa Sayuni,  
kwa maana mkuu ni yeye Aliye Mtakatifu wa Israeli miongoni mwenu.”