15
Unabii dhidi ya Moabu 
  1 Neno la unabii kuhusu Moabu:  
Ari iliyo Moabu imeangamizwa:  
imeharibiwa kwa usiku mmoja!  
Kiri iliyo Moabu imeangamizwa,  
imeharibiwa kwa usiku mmoja!   
 2 Diboni anakwea hadi kwenye hekalu lake,  
hadi mahali pake pa juu pa kuabudia ili walie,  
Moabu anaombolezea Nebo na Medeba.  
Kila kichwa kimenyolewa  
na kila ndevu limeondolewa.   
 3 Wamevaa magunia barabarani;  
juu ya mapaa na kwenye viwanja  
wote wanaomboleza,  
wakilala kifudifudi na kulia.   
 4 Heshboni na Eleale wanalia,  
sauti zao zinasikika hadi Yahazi.  
Kwa hiyo watu wenye silaha wa Moabu wanapiga kelele,  
nayo mioyo yao imezimia.   
 5 Moyo wangu unamlilia Moabu;  
wakimbizi wake wanakimbilia Soari,  
hadi Eglath-Shelishiya.  
Wanapanda njia ya kwenda Luhithi,  
wanaenda huku wanalia;  
barabarani iendayo Horonaimu  
wanaombolezea maangamizi yao.   
 6 Maji ya Nimrimu yamekauka  
na majani yamenyauka;  
mimea imekauka wala hakuna  
kitu chochote kibichi kilichobaki.   
 7 Kwa hiyo mali waliyoipata na kujiwekea akiba  
wamezichukua na kuvuka Bonde la Mierebi.   
 8 Mwangwi wa kilio chao umefika hadi mpakani mwa Moabu,  
kilio chao cha huzuni kimefika hadi Eglaimu,  
maombolezo yao hadi Beer-Elimu.   
 9 Maji ya Dimoni yamejaa damu,  
lakini bado nitaleta pigo jingine juu ya Dimoni:  
simba juu ya wakimbizi wa Moabu  
na juu ya wale wanaobaki katika nchi.