31
Ole wa wale wanaotegemea Misri
Ole wao wale wanaoshuka Misri kutafuta msaada,
wale wanaotegemea farasi,
wanaoweka tumaini katika wingi wa magari yao ya vita,
na katika nguvu nyingi za wapanda farasi,
lakini hawamwangalii yeye Aliye Mtakatifu wa Israeli,
wala hawatafuti msaada kwa Mwenyezi Mungu.
Hata hivyo yeye pia ana hekima na anaweza kuleta maafa,
wala hayatangui maneno yake.
Yeye atainuka dhidi ya nyumba ya mwovu,
dhidi ya wale ambao huwasaidia watenda maovu.
Lakini Wamisri ni wanadamu, wala si Mungu,
farasi wao ni nyama, wala si roho.
Mwenyezi Mungu atakaponyoosha Mkono wake,
yeye anayesaidia atajikwaa,
naye anayesaidiwa ataanguka,
wote wawili wataangamia pamoja.
Hili ndilo Mwenyezi Mungu analoniambia:
“Kama vile simba angurumavyo,
simba mkubwa juu ya mawindo yake:
hata ingawa kundi lote la wafugaji
huitwa pamoja dhidi yake,
hatiwi hofu na kelele zao,
wala kusumbuliwa na ghasia zao;
ndivyo Mwenyezi Mungu,
Mungu wa majeshi ya mbinguni atakavyoshuka
kufanya vita juu ya Mlima Sayuni
na juu ya vilele vyake.
Kama ndege warukao,
Mwenyezi Mungu, Mungu wa majeshi ya mbinguni
ataukinga Yerusalemu;
ataukinga na kuuokoa,
atapita juu yake na kuufanya salama.”
Mrudieni yeye ambaye nyumba ya Israeli imemwasi sana. Kwa kuwa katika siku ile kila mmoja wenu atazikataa sanamu za fedha na za dhahabu zilizotengenezwa kwa mikono yenu yenye dhambi.
“Ashuru itaanguka kwa upanga ambao si wa mwanadamu;
upanga usio wa kibinadamu utawaangamiza.
Watakimbia mbele ya upanga
na vijana wao wa kiume watafanyizwa kazi kwa lazima.
Ngome zao zitaanguka kwa sababu ya hofu;
kwa kuona bendera ya vita,
majemadari wao watashikwa na hofu ya ghafula,”
asema Mwenyezi Mungu,
ambaye moto wake uko Sayuni,
nalo tanuru lake liko Yerusalemu.