46
Miungu ya Babeli
Beli anasujudu, Nebo anainama;
sanamu zao zabebwa na wanyama wa mizigo.
Vinyago hivi mnavyobeba kila mahali ni mzigo wa kulemea,
mzigo kwa waliochoka.
Vinyago pamoja na wale wanaovibeba wanainama chini;
hiyo miungu haiwezi kuwaokoa watu,
wote wanaenda utumwani pamoja.
 
“Nisikilizeni mimi, ee nyumba ya Yakobo,
ninyi nyote mliobaki wa nyumba ya Israeli,
ninyi ambao nimewategemeza tangu mlipotungwa mimba,
nami nimewabeba tangu kuzaliwa kwenu.
Hata wakati wa uzee wenu na mvi, Mimi ndiye,
Mimi ndiye nitakayewasaidia ninyi.
Nimewahuluku, nami nitawabeba,
nitawahudumia ninyi na kuwaokoa.
 
“Mtanilinganisha na nani,
au mtanihesabu kuwa sawa na nani?
Ni nani mtakayenifananisha naye
ili tuweze kulinganishwa?
Wengine humwaga dhahabu kutoka mifuko yao,
na kupima fedha kwenye mizani;
huajiri mfua dhahabu kutengeneza mungu,
kisha huisujudia na kuiabudu.
Huiinua mabegani na kuichukua;
huiweka mahali pake, papo hapo ndipo isimamapo.
Wala haiwezi kusogea kutoka mahali pale.
Ingawa mtu huililia, haimjibu;
haiwezi kumwokoa kwenye taabu zake.
 
“Kumbukeni hili, litieni akilini,
liwekeni moyoni, enyi waasi.
Kumbukeni mambo yaliyopita, yale ya zamani za kale;
mimi ndimi Mungu, wala hakuna mwingine;
mimi ndimi Mungu,
wala hakuna mwingine aliye kama mimi.
10 Ni mimi nitangazaye mwisho tangu mwanzo,
naam, tangu zamani za kale,
mambo ambayo hayajatendeka.
Ninasema: Kusudi langu ndilo litakalosimama,
nami nitatenda mapenzi yangu yote.
11 Kutoka mashariki ninaita ndege awindaye;
kutoka nchi ya mbali,
mtu atakayetimiza kusudi langu.
Lile ambalo nimelisema, ndilo nitakalolitimiza;
lile nililolipanga, ndilo nitakalolitenda.
12 Nisikilizeni, ninyi wenye mioyo migumu,
ninyi mlio mbali na haki.
13 Ninaleta haki yangu karibu,
haiko mbali;
wala wokovu wangu hautachelewa.
Nitawapa Sayuni wokovu,
Israeli utukufu wangu.