2
Maombi ya Yona na kuokolewa
1 Akiwa ndani ya tumbo la samaki, Yona alimwomba Mwenyezi Mungu, Mungu wake. 2 Akasema:
“Katika shida yangu nalimwita Mwenyezi Mungu,
naye akanijibu.
Kutoka kina cha kaburi*Kaburi hapa maana yake ni Kuzimu; kwa Kiebrania ni Sheol. niliomba msaada,
nawe ukasikiliza kilio changu.
3 Ulinitupa kwenye kilindi,
ndani kabisa ya moyo wa bahari,
mikondo ya maji ilinizunguka;
mawimbi yako yote na viwimbi
vilipita juu yangu.
4 Nikasema, ‘Nimefukuziwa
mbali na uso wako,
hata hivyo nitatazama tena
kuelekea Hekalu lako takatifu.’
5 Maji yaliyonimeza yalinitisha,
kilindi kilinizunguka;
mwani ulijisokota kichwani pangu.
6 Nilizama chini sana hata pande za mwisho za milima,
makomeo ya hiyo nchi yalinifungia hata milele.
Lakini uliuleta uhai wangu kutoka shimoni,
Ee Mwenyezi Mungu, Mungu wangu.
7 “Uhai wangu ulipokuwa unatoka,
nilikukumbuka wewe, Mwenyezi Mungu,
nayo maombi yangu yalikufikia wewe,
katika Hekalu lako takatifu.
8 “Wale watu wanaoshikilia sanamu batili
hupoteza neema yao.
9 Lakini mimi nitakutolea dhabihu,
kwa sauti za shukrani na shangwe.
Lile nililowekea nadhiri nitalitimiza.
Wokovu watoka kwa Mwenyezi Mungu.”
10 Basi Mwenyezi Mungu akamwamuru yule samaki, naye akamtapika Yona katika nchi kavu.