Mathayo
Maisha na huduma ya awali ya Isa
1
(Mathayo 1–4)
Kumbukumbu za ukoo wa Isa Al-Masihi
(Luka 3:23-38)
Habari za ukoo wa Isa Al-Masihi mwana wa Daudi*Mariamu, mamake Isa, na pia Yusufu, baba mlezi wa Isa, walitokea ukoo wa Mfalme Daudi. Ina maana kwamba Isa ni mrithi wa kiti cha enzi cha Mwenyezi Mungu (Zaburi 89:3-4)., mwana wa Ibrahimu:
 
Ibrahimu akamzaa Isaka,
Isaka akamzaa Yakobo,
Yakobo akawazaa Yuda na ndugu zake,
Yuda akawazaa Peresi na Zera, ambao mama yao alikuwa Tamari,
Peresi akamzaa Esromu,
Esromu akamzaa Aramu,
Aramu akamzaa Aminadabu,
Aminadabu akamzaa Nashoni,
Nashoni akamzaa Salmoni,
Salmoni akamzaa Boazi, na mama yake Boazi alikuwa Rahabu,
Boazi akamzaa Obedi, ambaye mama yake alikuwa Ruthu,
Obedi akamzaa Yese,
Yese akamzaa Daudi, aliyekuwa mfalme.
 
Daudi akamzaa Sulemani, ambaye mama yake ni yule aliyekuwa mke wa Uria.
Sulemani akamzaa Rehoboamu,
Rehoboamu akamzaa Abiya,
Abiya akamzaa Asa,
Asa akamzaa Yehoshafati,
Yehoshafati akamzaa Yoramu,
Yoramu akamzaa Uzia,
Uzia akamzaa Yothamu,
Yothamu akamzaa Ahazi,
Ahazi akamzaa Hezekia,
10 Hezekia akamzaa Manase,
Manase akamzaa Amoni,
Amoni akamzaa Yosia,
11 wakati wa uhamisho wa Babeli, Yosia alimzaa Yekonia na ndugu zake.
 
12 Baada ya uhamisho wa Babeli:
Yekonia alimzaa Shealtieli,
Shealtieli akamzaa Zerubabeli,
13 Zerubabeli akamzaa Abihudi,
Abihudi akamzaa Eliakimu,
Eliakimu akamzaa Azori,
14 Azori akamzaa Sadoki,
Sadoki akamzaa Akimu,
Akimu akamzaa Eliudi,
15 Eliudi akamzaa Eleazari,
Eleazari akamzaa Matani,
Matani akamzaa Yakobo,
16 naye Yakobo akamzaa Yusufu, aliyekuwa mumewe Mariamu, mama yake Isa, aitwaye Al-Masihi.Al-Masihi maana yake Aliyetiwa mafuta.
 
17 Hivyo, kulikuwa na jumla ya vizazi kumi na vinne tangu Ibrahimu hadi Daudi, vizazi kumi na vinne tangu Daudi hadi wakati wa uhamisho wa Babeli, na vizazi kumi na vinne tangu wakati wa uhamisho wa Babeli hadi Al-Masihi.
Kuzaliwa kwa Isa
(Luka 2:1-7)
18 Kuzaliwa kwake Isa Al-Masihi kulikuwa hivi: Mariamu mama yake alikuwa ameposwa na Yusufu, lakini kabla hawajakutana kimwili, Mariamu alionekana kuwa na mimba kwa uweza wa Roho Mtakatifu wa Mungu. 19 Kwa kuwa Yusufu, mwanaume aliyekuwa amemposa alikuwa mtu mwadilifu, hakutaka kumwaibisha Mariamu hadharani, hivyo basi alikusudia kumwacha kwa siri.
20 Lakini alipokuwa akifikiri kufanya jambo hili, malaika wa Mwenyezi Mungu akamtokea katika ndoto na kusema, “Yusufu mwana wa Daudi, usiogope kumchukua Mariamu awe mke wako, kwa maana mimba aliyo nayo ni kwa uweza wa Roho wa Mungu. 21 Naye atamzaa mwana, nawe utamwita jina IsaIsa ni Iesous kwa Kiyunani, na kwa Kiebrania ni Yoshua au Yeshua; maana yake Yehova ni wokovu., kwa maana yeye ndiye atakayewaokoa watu wake kutoka dhambi zao.”
22 Haya yote yalitukia ili litimie lile Mwenyezi Mungu alilonena kupitia nabii, aliposema: 23 “Tazama, bikira atachukua mimba, naye atamzaa mwana, nao watamwita jina Imanueli” (maana yake, “Mungu pamoja nasi”).
24 Yusufu alipoamka kutoka usingizini, akafanya jinsi alivyoagizwa na malaika wa Mwenyezi Mungu, akamchukua Mariamu kuwa mke wake. 25 Lakini hawakukutana kimwili hadi Mariamu alipojifungua mwanawe§tafsiri zingine husema kifungua mimba; akamwita jina Isa.

*1:1 Mariamu, mamake Isa, na pia Yusufu, baba mlezi wa Isa, walitokea ukoo wa Mfalme Daudi. Ina maana kwamba Isa ni mrithi wa kiti cha enzi cha Mwenyezi Mungu (Zaburi 89:3-4).

1:16 Al-Masihi maana yake Aliyetiwa mafuta.

1:21 Isa ni Iesous kwa Kiyunani, na kwa Kiebrania ni Yoshua au Yeshua; maana yake Yehova ni wokovu.

§1:25 tafsiri zingine husema kifungua mimba