Zaburi
Kitabu cha Kwanza
1
(Zaburi 1–41)
Furaha ya kweli
1 Heri mtu yule ambaye haendi
katika shauri la watu waovu,
wala hasimami katika njia ya wenye dhambi,
au kuketi katika baraza la wenye mizaha.
2 Bali huifurahia Torati ya Mwenyezi Mungu,
naye huitafakari hiyo Torati usiku na mchana.
3 Mtu huyo ni kama mti uliopandwa
kando ya vijito vya maji,
ambao huzaa matunda kwa majira yake
na majani yake hayanyauki.
Lolote afanyalo hufanikiwa.
Huzuni ya waovu
4 Sivyo walivyo waovu!
Wao ni kama makapi
yanayopeperushwa na upepo.
5 Kwa hiyo waovu hawatastahimili hukumu,
wala wenye dhambi katika kusanyiko la wenye haki.
6 Kwa maana Mwenyezi Mungu huziangalia njia za mwenye haki,
bali njia za waovu zitaangamia.