Zaburi 4
Sala ya jioni ya kuomba msaada 
 Kwa mwimbishaji. Kwa ala za nyuzi za muziki. Zaburi ya Daudi. 
  1 Nijibu nikuitapo,  
Ee Mungu wangu mwenye haki!  
Nipumzishe katika shida zangu;  
nirehemu, usikie ombi langu.   
 2 Enyi watu, mtabadilisha utukufu wangu  
kuwa aibu hadi lini?  
Mtapenda udanganyifu  
na kufuata miungu ya uongo hadi lini?   
 3 Fahamuni hakika kwamba Mwenyezi Mungu amewatenga  
wale wamchao kwa ajili yake;  
Mwenyezi Mungu atanisikia nimwitapo.   
 4 Katika hasira yako, usitende dhambi.  
Tulieni kimya mkiwa vitandani mwenu,  
mkiichunguza mioyo yenu.   
 5 Toeni dhabihu zilizo haki;  
mtegemeeni Mwenyezi Mungu.   
 6 Wengi wanauliza, “Ni nani awezaye  
kutuonesha jema lolote?”  
Ee Mwenyezi Mungu, tuangazie nuru ya uso wako.   
 7 Wewe umejaza moyo wangu kwa furaha kubwa  
kuliko watu waliopata nafaka na divai kwa wingi.   
 8 Nitajilaza chini na kulala kwa amani,  
kwa kuwa wewe peke yako, Ee Mwenyezi Mungu,  
waniwezesha kukaa kwa salama.