Zaburi 6
Sala ya kuomba msaada wakati wa taabu
Kwa mwimbishaji. Kwa ala za nyuzi za muziki. Mtindo wa sheminithi.*Sheminithi ni mtajo mmojawapo katika lugha ya uimbaji. Zaburi ya Daudi.
Ee Mwenyezi Mungu, usinikemee katika hasira yako,
wala usiniadhibu katika ghadhabu yako.
Unirehemu Mwenyezi Mungu,
kwa maana nimedhoofika;
Ee Mwenyezi Mungu, uniponye,
kwa maana mifupa yangu
ina maumivu makali.
Nafsi yangu ina uchungu mwingi.
Hadi lini, Ee Mwenyezi Mungu, hadi lini?
 
Geuka, Ee Mwenyezi Mungu, unikomboe,
uniokoe kwa sababu ya fadhili zako.
Hakuna mtu anayekukumbuka
akiwa amekufa.
Ni nani awezaye kukusifu
akiwa KuzimuKuzimu kwa Kiebrania ni Sheol, yaani Shimo lisilo na mwisho.?
 
Nimechakaa kwa kulia kwa huzuni;
usiku kucha natiririsha
kitanda changu kwa machozi;
nimelowesha kiti changu
kwa machozi yangu.
Macho yangu yamedhoofika kwa kuhuzunika,
yamedhoofika kwa sababu ya adui zangu wote.
 
Kaeni mbali nami, ninyi nyote mtendao mabaya,
kwa maana Mwenyezi Mungu amesikia kulia kwangu.
Mwenyezi Mungu amesikia kilio changu kwa huruma,
Mwenyezi Mungu amekubali sala yangu.
10 Adui zangu wote wataaibika na kufadhaika,
watarudi nyuma na waaibishwe kwa ghafula.

*^ Sheminithi ni mtajo mmojawapo katika lugha ya uimbaji.

Zaburi 6:5 Kuzimu kwa Kiebrania ni Sheol, yaani Shimo lisilo na mwisho.