Zaburi 70
Kuomba msaada 
 (Zaburi 40:13-17)  
Kwa mwimbishaji. Zaburi ya Daudi. Maombi. 
  1 Ee Mungu, ufanye haraka kuniokoa;  
Ee Mwenyezi Mungu, njoo hima unisaidie.   
 2 Wale wanaotafuta kuniua,  
waaibishwe na kufadhaishwa;  
wote wanaotamani kuangamizwa kwangu,  
warudishwe nyuma kwa aibu.   
 3 Wale wanaoniambia, “Aha! Aha!”  
na warudi nyuma kwa sababu ya aibu yao.   
 4 Lakini wote wanaokutafuta  
washangilie na kukufurahia,  
wale wanaoupenda wokovu wako siku zote waseme,  
“Mwenyezi Mungu ni mkuu!”   
 5 Lakini mimi bado ni maskini na mhitaji;  
Ee Mungu, unijie haraka.  
Wewe ndiwe msaada wangu na mwokozi wangu;  
Ee Mwenyezi Mungu, usikawie.