Zaburi 84
Kuionea shauku nyumba ya Mwenyezi Mungu 
 Kwa mwimbishaji. Mtindo wa gitithi. Zaburi ya wana wa Kora. 
  1 Ee Mwenyezi Mungu, Mungu wa majeshi ya mbinguni,  
makao yako yapendeza kama nini!   
 2 Nafsi yangu inatamani sana,  
naam, hata kuona shauku,  
kwa ajili ya nyua za Mwenyezi Mungu;  
moyo wangu na mwili wangu  
vinamlilia Mungu Aliye Hai.   
 3 Hata shomoro amejipatia makao,  
mbayuwayu amejipatia kiota  
mahali awezapo kuweka makinda yake:  
mahali karibu na madhabahu yako,  
Ee Mwenyezi Mungu, Mungu wa majeshi ya mbinguni,  
Mfalme wangu na Mungu wangu.   
 4 Heri wale wanaokaa nyumbani mwako,  
wanaokusifu wewe daima.   
 5 Heri wale ambao nguvu zao ziko kwako,  
na njia ziendazo Sayuni zimo mioyoni mwao.   
 6 Wanapopita katika Bonde la Baka*maana yake Bonde la Vilio,  
hulifanya mahali pa chemchemi,  
pia mvua za vuli hulijaza kwa madimbwi†au baraka.   
 7 Huendelea toka nguvu hadi nguvu,  
hadi kila mmoja afikapo  
mbele za Mungu huko Sayuni.   
 8 Ee Bwana Mwenyezi Mungu,  
Mungu wa majeshi ya mbinguni,  
sikia maombi yangu;  
nisikilize, Ee Mungu wa Yakobo.   
 9 Ee Mungu, uitazame ngao yetu,  
mtazame kwa wema mpakwa mafuta wako.   
 10 Siku moja katika nyua zako ni bora  
kuliko siku elfu mahali pengine;  
afadhali ningekuwa bawabu katika nyumba ya Mungu wangu  
kuliko kukaa katika mahema ya waovu.   
 11 Kwa kuwa Bwana Mwenyezi Mungu ni jua na ngao;  
Mwenyezi Mungu hutoa wema na heshima;  
hakuna kitu chema anachowanyima  
wale ambao hawana hatia.   
 12 Ee Mwenyezi Mungu, Mungu wa majeshi ya mbinguni,  
heri mtu anayekutumaini wewe.