Zaburi 141
Maombi ya kuhifadhiwa dhidi ya uovu 
 Zaburi ya Daudi. 
  1 Ee Mwenyezi Mungu, ninakuita, njoo kwangu hima.  
Sikia sauti yangu ninapokuita.   
 2 Maombi yangu na yafike mbele zako kama uvumba;  
kuinua mikono yangu juu na kuwe kama dhabihu ya jioni.   
 3 Ee Mwenyezi Mungu, weka mlinzi kinywani mwangu,  
weka ulinzi mlangoni mwa midomo yangu.   
 4 Usiuache moyo wangu uvutwe katika jambo baya,  
nisije nikashiriki katika matendo maovu  
pamoja na watu watendao mabaya,  
wala nisije nikala vyakula vyao vya anasa.   
 5 Mtu mwenye haki na anipige: ni jambo la huruma;  
na anikemee: ni mafuta kichwani mwangu.  
Kichwa changu hakitalikataa.  
Hata hivyo, maombi yangu daima  
ni kinyume cha watenda maovu.   
 6 Watawala wao watatupwa chini  
kutoka majabali,  
waovu watajifunza kwamba maneno yangu  
yalikuwa kweli.   
 7 Watasema, “Kama mtu anavyolima na kuvunja ardhi,  
ndivyo mifupa yetu imetawanywa kwenye mlango wa kaburi.”   
 8 Lakini nimekaza macho yangu kwako, Ee Bwana Mungu Mwenyezi,  
ndani yako nimekimbilia, usiniache nife.   
 9 Niepushe na mitego waliyonitegea,  
kutokana na mitego iliyotegwa na watenda maovu.   
 10 Waovu na waanguke kwenye nyavu zao wenyewe,  
wakati mimi ninapita salama.