Zaburi 146
Kumsifu Mwenyezi Mungu mwokozi 
  1 Msifuni Mwenyezi Mungu!*kwa Kiebrania ni Hallelu Yah; pia 146:10.  
Ee nafsi yangu, umsifu Mwenyezi Mungu,   
 2 Nitamsifu Mwenyezi Mungu maisha yangu yote;  
nitamwimbia Mungu wangu sifa  
wakati wote ningali hai.   
 3 Usiweke tumaini lako kwa wakuu,  
kwa wanadamu ambao hufa,  
ambao hawawezi kuokoa.   
 4 Roho yao itokapo hurudi mavumbini,  
siku hiyo hiyo mipango yao yote hukoma.   
 5 Heri yeye ambaye Mungu wa Yakobo ni msaada wake,  
ambaye tumaini lake ni katika Mwenyezi Mungu, Mungu wake,   
 6 Muumba wa mbingu na nchi,  
na bahari na vyote vilivyomo:  
Mwenyezi Mungu anayedumu kuwa mwaminifu  
milele na milele.   
 7 Naye huwapatia haki waliodhulumiwa,  
na kuwapa wenye njaa chakula.  
Mwenyezi Mungu huwaweka wafungwa huru,   
 8 Mwenyezi Mungu huwafumbua vipofu macho,  
Mwenyezi Mungu huwainua waliolemewa na mizigo yao,  
Mwenyezi Mungu huwapenda wenye haki.   
 9 Mwenyezi Mungu huwalinda wageni  
na kuwategemeza yatima na wajane,  
lakini hupinga njia za waovu.   
 10 Mwenyezi Mungu atamiliki milele,  
Mungu wako, ee Sayuni,  
kwa vizazi vyote.  
Msifuni Mwenyezi Mungu.