2
Hukumu dhidi ya mataifa
Dhidi ya Yuda
1 Kusanyikeni pamoja, kusanyikeni pamoja,
enyi taifa lisilo na aibu,
2 kabla wakati ulioamriwa haujafika
na siku ile inayopeperusha kama makapi,
kabla hasira kali ya Mwenyezi Mungu haijaja juu yenu,
kabla siku ya ghadhabu ya Mwenyezi Mungu
haijaja juu yenu.
3 Mtafuteni Mwenyezi Mungu, enyi nyote wanyenyekevu wa nchi,
ninyi ambao hufanya lile analoamuru.
Tafuteni haki, tafuteni unyenyekevu;
labda mtahifadhiwa
siku ya hasira ya Mwenyezi Mungu.
Dhidi ya Ufilisti
4 Gaza utaachwa
na Ashkeloni utaachwa magofu.
Wakati wa adhuhuri Ashdodi utaachwa mtupu,
na Ekroni utang’olewa.
5 Ole wenu ninyi ambao mnaishi kando ya bahari,
enyi Wakerethi;
neno la Mwenyezi Mungu liko dhidi yenu,
ee Kanaani, nchi ya Wafilisti.
“Mimi nitawaangamiza,
na hakuna atakayebaki.”
6 Nchi iliyo karibu na bahari itakuwa malisho
yenye visima vya wachungaji,
na mazizi ya kondoo.
7 Itakuwa mali ya mabaki ya nyumba ya Yuda,
hapo watapata malisho.
Wakati wa jioni watajilaza chini
katika nyumba za Ashkeloni.
Mwenyezi Mungu, Mungu wao, atawatunza,
naye atawarudishia wafungwa wao.
Dhidi ya Moabu na Amoni
8 “Nimeyasikia matukano ya Moabu
nazo dhihaka za Waamoni,
ambao waliwatukana watu wangu
na kutoa vitisho dhidi ya nchi yao.
9 Hakika, kama niishivyo,”
asema Mwenyezi Mungu, Mungu wa majeshi ya mbinguni,
Mungu wa Israeli,
“hakika Moabu itakuwa kama Sodoma,
Waamoni kama Gomora:
mahali pa magugu na mashimo ya chumvi,
nchi ya ukiwa milele.
Mabaki ya watu wangu watawateka nyara;
mabaki ya taifa langu watarithi nchi yao.”
10 Hiki ndicho watarudishiwa kwa ajili ya kiburi chao,
kwa kutukana na kudhihaki
watu wa Mwenyezi Mungu,
Mungu wa majeshi ya mbinguni.
11 Mwenyezi Mungu atakuwa wa kuhofisha kwao
atakapoangamiza miungu yote ya nchi.
Mataifa katika kila pwani yatamwabudu,
kila moja katika nchi yake.
Dhidi ya Kushi
12 “Ninyi pia, ee Wakushi,
mtauawa kwa upanga wangu.”
Dhidi ya Ashuru
13 Mungu atanyoosha mkono wake dhidi ya kaskazini
na kuangamiza Waashuru,
akiiacha Ninawi ukiwa
na pakame kama jangwa.
14 Makundi ya kondoo na ng’ombe yatajilaza pale,
viumbe vya kila aina.
Bundi wa jangwani na bundi waliao kwa sauti nyembamba
wataishi juu ya nguzo zake.
Mwangwi wa kuita kwao utapita madirishani,
kifusi kitakuwa milangoni,
boriti za mwerezi zitaachwa wazi.
15 Huu ndio mji uliotukuka na kuishi kwa furaha
wakijisikia salama.
Ulisema moyoni mwako,
“Mimi ndimi, na wala hapana mwingine ila mimi.”
Jinsi gani umekuwa gofu,
mahali pa kulala wanyama pori!
Wote wanaopita kando yake wanauzomea
na kutikisa mkono kwa dharau.