22
Yesu alisema nao tena kwa kutumia mifano: “Ufalme wa mbinguni umefanana na mfalme aliyemwandalia mwanawe karamu ya arusi. Basi, akawatuma watumishi kuwaita walioalikwa waje arusini, lakini walioalikwa hawakutaka kufika. Akawatuma tena watumishi wengine, akisema, Waambieni wale walioalikwa: karamu yangu iko tayari sasa; fahali wangu na ng'ombe wanono wamekwisha chinjwa; kila kitu ni tayari, njoni arusini. Lakini wao hawakujali, wakaenda zao; mmoja shambani kwake, mwingine kwenye shughuli zake, na wengine wakawakamata wale watumishi wakawatukana, wakawaua. Yule mfalme akakasirika, akawatuma askari wake wakawaangamize wauaji hao na kuuteketeza mji wao. Kisha akawaambia watumishi wake: Karamu ya arusi iko tayari kweli, lakini walioalikwa hawakustahili. Basi, nendeni kwenye barabara na wowote wale mtakaowakuta waiteni waje arusini. 10 Wale watumishi wakatoka, wakaenda njiani, wakawaleta watu wote, wabaya na wema. Nyumba ya arusi ikajaa wageni. 11 “Mfalme alipoingia kuwaona wageni, akamwona mtu mmoja ambaye hakuvaa mavazi ya arusi. 12 Mfalme akamwuliza, Rafiki, umeingiaje hapa bila vazi la arusi? Lakini yeye akakaa kimya. 13 Hapo mfalme akawaambia watumishi, Mfungeni miguu na mikono mkamtupe nje gizani; huko atalia na kusaga meno.” 14 Yesu akamaliza kwa kusema, “Wengi wamealikwa, lakini wachache wameteuliwa.” 15 Kisha, Mafarisayo wakaenda zao, wakashauriana jinsi ya kumnasa Yesu kwa maneno yake. 16 Basi, wakawatuma wafuasi wao pamoja na wafuasi wa kikundi cha Herode. Wakamwuliza, “Mwalimu, tunajua kwamba wewe ni mtu mwaminifu, na kwamba wafundisha njia ya Mungu kwa uaminifu; humwogopi mtu yeyote, maana cheo cha mtu si kitu kwako. 17 Haya, twambie maoni yako. Je, ni halali au la, kulipa Kaisari?” 18 Lakini Yesu alitambua uovu wao, akawaambia, “Enyi 19 Nionyesheni fedha ya kulipia kodi.” Nao wakamtolea sarafu ya fedha. sarafu ya fedha. 20 Basi, Yesu akawauliza, “Sura na chapa hii ni ya nani?” 21 Wakamjibu, “Ni vya Kaisari.” Hapo Yesu akawaambia, “Basi, mpeni Kaisari yaliyo yake Kaisari, na Mungu yaliyo yake Mungu.” 22 Waliposikia hivyo wakashangaa; wakamwacha, wakaenda zao. 23 Siku hiyo, baadhi ya Masadukayo walimwendea Yesu. Hao ndio wale wasemao kwamba wafu hawafufuki. 24 Basi, wakamwambia, “Mwalimu, Mose alisema mtu aliyeoa akifa bila kuacha watoto, lazima ndugu yake amwoe huyo mama mjane, amzalie ndugu yake watoto. 25 Sasa, hapa petu palikuwa na ndugu saba. Wa kwanza alioa kisha akafa bila kujaliwa watoto, akamwachia ndugu yake huyo mke wake mjane. 26 Ikawa vivyo hivyo kwa ndugu wa pili, na wa tatu, mpaka wa saba. 27 Baada ya ndugu hao wote kufa, akafa pia yule mama. 28 Je, siku wafu watakapofufuka mama huyo atakuwa mke wa nani miongoni mwa wale ndugu saba? Maana Wote saba walimwoa.” 29 Yesu akawajibu, “Kweli mmekosea kwa sababu hamjui Maandiko Matakatifu wala nguvu ya Mungu! 30 Maana wafu watakapofufuliwa hawataoa wala kuolewa, watakuwa kama malaika mbinguni. 31 Lakini kuhusu suala la wafu kufufuka, hamjasoma yale aliyowaambieni Mungu? 32 Aliwaambia, Mimi ni Mungu wa Abrahamu, Isaka na Yakobo! Basi, yeye si Mungu wa wafu, bali ni Mungu wa walio hai.” 33 Ule umati wa watu uliposikia hivyo ukayastaajabia mafundisho yake. 34 Mafarisayo waliposikia kwamba Yesu alikuwa amewanyamazisha Masadukayo, wakakutana pamoja. 35 Mmoja wao, mwanasheria, akamwuliza Yesu kwa kumjaribu, 36 “Mwalimu, ni amri ipi iliyo kuu katika Sheria ya Mose?” 37 Yesu akamjibu, “Mpende Bwana Mungu wako kwa moyo wako wote, kwa roho yako yote na kwa akili yako yote. 38 Hii ndiyo amri kuu ya kwanza. 39 Ya pili inafanana na hiyo: Mpende jirani yako kama unavyojipenda wewe mwenyewe. 40 Sheria yote ya Mose na mafundisho ya manabii vinategemea amri hizi mbili.” 41 Mafarisayo walipokusanyika pamoja, Yesu aliwauliza, 42 “Ninyi mwaonaje juu ya Kristo? Je, ni mwana wa nani?” Wakamjibu, “Wa Daudi.” 43 Yesu akawaambia, “Basi, inawezekanaje kwamba kwa nguvu ya Roho Mtakatifu Daudi anamwita yeye Bwana? Maana alisema: 44 Bwana alimwambia Bwana wangu: keti upande wangu wa kulia, mpaka niwaweke adui zako chini ya miguu yako. 45 Basi, ikiwa Daudi anamwita Kristo Bwana, anawezaje kuwa mwanawe?” 46 Hakuna mtu yeyote aliyeweza kumjibu neno. Na tangu siku hiyo hakuna aliyethubutu tena kumwuliza swali.