24
Ayubu Analalamikia Jeuri Duniani
“Kwa nini Mwenyezi asiweke nyakati kwa ajili ya hukumu?
Kwa nini wale wamjuao wazitafute siku kama hizo bila mafanikio?
Watu husogeza mawe ya mpaka;
huchunga makundi ya wanyama waliyonyangʼanya kwa nguvu.
Huwanyangʼanya yatima punda wao,
na kumchukua rehani fahali wa mjane.
Humsukuma mhitaji kutoka njia,
na kuwafanya maskini wote wa nchi kulazimika kujificha.
Kama punda-mwitu jangwani,
maskini huzunguka katika kazi zao za kutafuta chakula;
mahali palipo jangwa
huwapa chakula cha watoto wao.
Hukusanya chakula mashambani na kuokota masazo
katika mashamba ya mizabibu ya waovu.
Kwa kukosa nguo, usiku kucha hukaa uchi;
hawana chochote cha kujifunika baridi.
Hutota kwa mvua za mlimani,
nao huikumbatia miamba kwa ajili ya kukosa pa kujisitiri.
Mtoto yatima hupokonywa matitini;
mtoto wachanga wa maskini hunyakuliwa kwa ajili ya deni.
10 Kwa kukosa nguo, hutembea uchi;
hubeba miganda ya ngano, lakini huwa na njaa.
11 Hukamua zeituni katika mawe ya kusagia;
hukanyaga mashinikizo, lakini wanaona kiu.
12 Kilio cha huzuni cha wanaokufa kinapaa kutoka mjini,
nazo nafsi za waliojeruhiwa zinalilia msaada.
Lakini Mungu hamlaumu mtu yeyote
kwa kutenda mabaya.
 
13 “Wako wale wanaoiasi nuru,
wasiofahamu njia zake
wala hawakai katika mapito yake.
14 Wakati mwanga wa mchana unapotoweka, muuaji huinuka
naye huwaua maskini na mhitaji;
wakati wa usiku hunyemelea kama mwizi.
15 Jicho la mzinzi hungojea wakati wa giza,
naye hufikiri, ‘Hakuna jicho litakaloniona,’
naye huuficha uso wake.
16 Katika giza, huvunja majumba,
lakini wakati wa mchana hujifungia ndani;
hawataki kufanya lolote nuruni.
17 Kwa wote hawa, giza nene ndiyo asubuhi yao;
hujifanya rafiki na vitisho vya gizani.
 
18 “Lakini wao ni povu juu ya maji;
sehemu yao juu ya nchi imelaaniwa,
hivyo hakuna hata mmoja
aendaye kwenye shamba la mizabibu.
19 Kama vile joto na hari vinyakuavyo theluji iliyoyeyuka,
ndivyo kuzimu kuwanyakuavyo waliotenda dhambi.
20 Tumbo lililowazaa huwasahau,
nao huwa karamu ya mabuu;
watu waovu hawakumbukwi tena,
lakini huvunjika kama mti.
21 Huwafanya mawindo wanawake tasa na wasio na watoto,
nao hawaonyeshi huruma kwa wajane.
22 Lakini Mungu huwakokota wenye nguvu kwa uwezo wake;
ingawa wamestawi, hawana hakika ya maisha.
23 Aweza akawaacha wakapumzika wakijihisi salama,
lakini macho yake yanaona njia zao.
24 Kwa kitambo kidogo hutukuka, hatimaye hutoweka;
hushushwa na kukusanywa kama wengine wote,
hukatwa kama masuke ya nafaka.
 
25 “Kama hili sivyo, ni nani awezaye kunithibitisha kuwa mwongo,
na kuyafanya maneno yangu kuwa si kitu?”