12
Mashujaa Waungana Na Daudi
Hawa ndio watu waliomjia Daudi huko Siklagi, wakati alikuwa amefukuzwa mbele ya Sauli mwana wa Kishi (walikuwa miongoni mwa mashujaa waliomsaidia Daudi vitani, walikuwa na pinde na walikuwa na uwezo wa kupiga mishale au kutupa mawe kwa kombeo wakitumia mkono wa kushoto au wa kulia; hawa walikuwa ndugu zake Sauli kutoka kabila la Benyamini):
Mkuu wao alikuwa Ahiezeri, na wa pili Yoashi, wote wana wa Shemaa Mgibeathi; pia Yezieli na Peleti wana wa Azmawethi; Beraka, Yehu Mwanathothi, na Ishmaya Mgibeoni, shujaa miongoni mwa wale Thelathini, ambaye alikuwa kiongozi wa wale Thelathini; Yeremia, Yahazieli, Yohanani, Yozabadi, Mgederathi, Eluzai, Yeremothi, Bealia, Shemaria, Shefatia, Mharufi; Elikana, Ishia, Azareli, Yoezeri na Yashobeamu, wana wa Kora; Yoela na Zebadia, wana wa Yerohamu, kutoka Gedori.
 
Baadhi ya Wagadi wakajitenga na kujiunga na Daudi katika ngome yake huko jangwani. Walikuwa mashujaa hodari, waliokuwa tayari kwa vita na wenye uwezo wa kutumia ngao na mkuki. Nyuso zao zilikuwa nyuso za simba na walikuwa na wepesi kama paa milimani.
Ezeri alikuwa mkuu wao,
Obadia alikuwa wa pili katika uongozi, Eliabu wa tatu,
10 Mishmana wa nne, Yeremia wa tano,
11 Atai wa sita, Elieli wa saba,
12 Yohanani wa nane, Elzabadi wa tisa,
13 Yeremia wa kumi, na Makbanai wa kumi na moja.
14 Hawa Wagadi walikuwa majemadari. Aliyekuwa wa mwisho kuliko wote aliweza kuongoza askari 100, na aliyekuwa na uweza zaidi ya wote aliongoza 1,000. 15 Wao ndio walivuka Mto Yordani katika mwezi wa kwanza ukiwa umefurika hadi kwenye kingo zake zote na kusababisha watu wote waliokuwa wanaishi kwenye mabonde kukimbilia mashariki na wengine magharibi.
16 Wabenyamini wengine na baadhi ya watu kutoka Yuda pia walikuja kwa Daudi katika ngome yake. 17 Daudi akatoka nje kuwalaki na akawaambia, “Kama mmekuja kwangu kwa amani, kunisaidia, mimi niko tayari kuwaruhusu ninyi kuungana nami. Lakini kama mmekuja ili kunisaliti kwa adui zangu wakati mimi mikono yangu haina hatia, basi Mungu wa baba zetu aone na awahukumu.”
18 Kisha Roho akaja juu ya Amasai, mkuu wa wale Thelathini, naye akasema:
“Sisi tu watu wako, ee Daudi!
Nasi tuko pamoja na wewe, ee mwana wa Yese!
Ushindi, naam, ushindi uwe kwako,
pia ushindi kwa wale walio upande wako,
kwa kuwa Mungu wako atakusaidia.”
Kwa hiyo Daudi akawapokea na kuwafanya viongozi wa vikosi vyake vya uvamizi.
19 Baadhi ya watu kutoka kabila la Manase wakajiunga na Daudi wakati alikwenda pamoja na Wafilisti, kupigana na Sauli. (Daudi na watu wake hawakuwasaidia Wafilisti kwa sababu, baada ya ushauri, watawala wao walimrudisha. Wakasema, “Itatugharimu vichwa vyetu kama Daudi atatuasi na kurudi kwa Sauli bwana wake.”) 20 Daudi alipokwenda Siklagi, hawa ndio watu wa kabila la Manase waliojiunga naye: Adna, Yozabadi, Yediaeli, Mikaeli, Yozabadi, Elihu na Silethai, viongozi wa vikosi vya watu 1,000 katika kabila la Manase. 21 Walimsaidia Daudi dhidi ya makundi ya uvamizi, kwa kuwa wote walikuwa mashujaa hodari na walikuwa majemadari katika jeshi lake. 22 Siku baada ya siku watu walikuja kumsaidia Daudi, mpaka akawa na jeshi kubwa, kama jeshi la Mungu.
Wengine Waungana Na Daudi Huko Hebroni
23 Hawa ndio watu waliojiandaa kwa ajili ya vita waliokuja kwa Daudi huko Hebroni ili kumtwalia ufalme kutoka kwa Sauli, kama Bwana alivyokuwa amesema:
24 watu wa Yuda, wanaochukua ngao na mikuki walikuwa 6,800 wote wakiwa tayari kwa vita.
25 Watu wa Simeoni, mashujaa waliokuwa tayari kwa vita walikuwa 7,100.
26 Watu wa Lawi walikuwa 4,600, 27 pamoja na Yehoyada, kiongozi wa jamaa ya Aroni, aliyekuwa pamoja na watu 3,700, 28 na Sadoki, kijana shujaa na hodari, aliyekuwa pamoja na maafisa ishirini na wawili kutoka jamaa yake.
29 Watu wa Benyamini, ndugu zake Sauli, walikuwa 3,000; wengi wao walikuwa wameendelea kuwa waaminifu kwa Sauli mpaka wakati huo.
30 Watu wa Efraimu, mashujaa hodari 20,800, watu waliokuwa maarufu katika koo zao.
31 Watu wa nusu ya kabila la Manase, waliotajwa kwa majina ili waje kumweka Daudi kuwa mfalme, watu 18,000.
32 Watu wa Isakari, waliofahamu majira na kujua kile ambacho Israeli inapasa kufanya, walikuwa viongozi 200, pamoja na jamaa zao wote chini ya uongozi wao.
33 Watu wa Zabuloni, askari wenye uzoefu mkubwa walioandaliwa tayari kwa vita wakiwa na silaha za kila aina, ili kumsaidia Daudi kwa uaminifu thabiti, walikuwa 50,000.
34 Watu wa Naftali, maafisa 1,000, pamoja na watu 37,000 waliochukua ngao na mikuki.
35 Watu wa Dani 28,600 waliokuwa tayari kwa vita.
36 Watu wa Asheri, askari 40,000 wenye uzoefu mkubwa waliondaliwa kwa ajili ya vita.
37 Na pia watu kutoka mashariki ya Yordani, watu wa Reubeni, Gadi na nusu ya kabila la Manase, wakiwa na kila aina ya silaha, watu 120,000.
38 Wote hawa walikuwa watu wapiganaji waliojitolea kutumika katika safu zao. Walikuja Hebroni wakiwa wameamua kikamilifu kumfanya Daudi mfalme juu ya Israeli yote. Waisraeli wengine wote walikuwa pia na nia hiyo moja ya kumfanya Daudi kuwa mfalme. 39 Watu hawa wakakaa huko na Daudi siku tatu, wakila na kunywa, kwa sababu jamaa zao zilikuwa zimewapatia mahitaji yao. 40 Pia, majirani zao hata wale walio mbali hadi Isakari, Zabuloni na Naftali, walikuja wakiwaletea vyakula walivyovibeba kwa punda, ngamia, nyumbu na maksai. Kulikuwepo na wingi wa unga, maandazi ya tini, maandazi ya zabibu kavu, divai, mafuta, ngʼombe na kondoo, kwa maana kulikuwa na furaha katika Israeli.