25
Daudi, Nabali na Abigaili
Basi Samweli akafa, nao Waisraeli wote wakakusanyika na kumwombolezea; wakamzika nyumbani mwake huko Rama.
Kisha Daudi akateremka kwenye Jangwa la Parani. Mtu mmoja huko Maoni, aliyekuwa na makao huko Karmeli, alikuwa tajiri sana. Alikuwa na mbuzi elfu moja na kondoo elfu tatu, aliokuwa akiwakata manyoya huko Karmeli. Jina la mtu huyo lilikuwa Nabali, naye mkewe aliitwa Abigaili. Alikuwa mwanamke mwenye busara na mzuri wa sura, lakini mumewe, aliyekuwa wa ukoo wa Kalebu, alikuwa mwenye hasira na mchoyo katika utendaji wake.
Daudi alipokuwa huko jangwani, akasikia kuwa Nabali alikuwa anakata kondoo manyoya. Basi akatuma vijana kumi na kuwaambia, “Pandeni kwa Nabali huko Karmeli, mkamsalimie kwa jina langu. Mwambieni: ‘Amani iwe kwako! Amani iwe kwako pamoja na wa nyumbani mwako! Pia amani iwe pamoja na vyote ulivyo navyo!
“ ‘Nasikia kuwa huu ni wakati wa kukata kondoo manyoya. Wafugaji wako walipokuwa pamoja nasi, hatukuwatendea mabaya na wakati wote waliokuwa huko Karmeli hakuna chochote chao kilipotea. Waulize watumishi wako nao watakuambia. Kwa hiyo uwatendee wema vijana wangu, kwani tumekuja wakati wa furaha. Tafadhali wape watumishi wako na mwanao Daudi chochote kitakachokuja mkononi mwako kwa ajili yao.’ ”
Watu wa Daudi walipofika wakampa Nabali ujumbe huu kwa jina la Daudi. Kisha wakangojea.
10 Nabali akawajibu watumishi wa Daudi, “Huyu Daudi ni nani? Huyu mwana wa Yese ni nani? Watumishi wengi wanakimbia kutoka kwa bwana zao siku hizi. 11 Kwa nini nichukue mkate wangu, maji yangu na nyama niliyochinja kwa ajili ya wakata manyoya wangu, na kuwapa watu ambao hakuna anayejua wanakotoka?”
12 Watu wa Daudi wakageuka na kurudi. Walipofika, wakaarifu kila neno. 13 Daudi akawaambia watu wake, “Jifungeni panga zenu!” Basi wakajifunga panga zao, naye Daudi akajifunga upanga wake. Watu kama mia nne hivi wakapanda pamoja na Daudi, na watu mia mbili wakabaki na vifaa.
14 Mmoja wa watumishi akamwambia Abigaili, mkewe Nabali: “Daudi alituma wajumbe kutoka jangwani kumpa bwana wetu salamu zake, lakini akawatukana. 15 Hata hivyo watu hawa walikuwa wema sana kwetu. Hawakututendea mabaya, na wakati wote tulipokuwa nje huko mashambani karibu nao, hatukupotewa na kitu chochote. 16 Usiku na mchana walikuwa ukuta wa ulinzi wakati wote tulipokuwa tukichunga kondoo wetu karibu nao. 17 Sasa fikiri juu ya jambo hili na uone unaweza kufanya nini, kwa sababu maafa yanakaribia juu ya bwana wetu na nyumba yake yote. Yeye ni mtu mwovu kiasi kwamba hakuna mtu awezaye kuzungumza naye.”
18 Abigaili akafanya haraka, akachukua mikate mia mbili, viriba viwili vya divai, kondoo watano waliochinjwa vipimo vitano vya bisi, vishada mia moja vya zabibu kavu, mikate mia mbili ya tini, akavipakia juu ya punda. 19 Kisha akawaambia watumishi wake, “Tangulieni; mimi nitakuja nyuma yenu.” Lakini hakumwambia Nabali mumewe.
20 Ikawa alipokuwa amepanda punda wake kwenye bonde la mlima, tazama, Daudi na watu wake wakawa wanateremka kumwelekea, naye akakutana nao. 21 Daudi alikuwa amesema, “Ilikuwa ni kazi bure kuchunga kwangu kote mali ya huyu mtu huko jangwani hivi kwamba hakuna chochote chake kilichopotea. Yeye amenilipa baya kwa ajili ya wema. 22 Mwenyezi Mungu na amwadhibu Daudi vikali zaidi, ikiwa kesho asubuhi nitambakizia mwanaume hata mmoja hai miongoni mwa watu wake wote!”
23 Abigaili alipomwona Daudi, akashuka haraka kwenye punda wake, akamsujudia Daudi. 24 Akamwangukia miguuni pake na kusema: “Bwana wangu, kosa hili na liwe juu yangu mwenyewe. Tafadhali mruhusu mtumishi wako aseme nawe. Sikia kile mtumishi wako atakachosema. 25 Bwana wangu na asimjali huyo mtu mwovu Nabali. Yeye anafanana na jina lake; jina lake ni Mpumbavu, nao upumbavu huenda pamoja naye. Lakini kwangu mimi, mtumishi wako, sikuwaona hao watu waliotumwa na bwana wangu.
26 “Basi sasa, bwana wangu, kwa kuwa Mwenyezi Mungu amekuzuia kumwaga damu na kulipiza kisasi kwa mikono yako mwenyewe, hakika kama Mwenyezi Mungu aishivyo na kama uishivyo, adui zako na wote wanaokusudia kumdhuru bwana wangu wawe kama Nabali. 27 Nayo zawadi hii ambayo mtumishi wako amemletea bwana wangu, wapewe watu wanaofuatana nawe. 28 Tafadhali samehe kosa la mtumishi wako, kwa kuwa Mwenyezi Mungu kwa hakika ataifanya imara nyumba ya ufalme kwa bwana wangu, kwa sababu anapigana vita vya Mwenyezi Mungu. 29 Hata ingawa kuna mtu anayekufuatia ili akuue, usiruhusu baya lolote kuonekana kwako siku zote za maisha yako, uhai wa bwana wangu utafungwa salama kwenye furushi la walio hai na Mwenyezi Mungu, Mungu wako. Lakini uhai wa adui zako utavurumishwa kama vile jiwe kutoka kombeo. 30 Mwenyezi Mungu atakapokuwa ameshamtendea bwana wangu kila kitu chema alichoahidi kumhusu na kumweka kuwa kiongozi wa Israeli, 31 bwana wangu hatakuwa na dhamiri inayolemewa na mzigo kwa kumwaga damu kusiko na sababu, au kujilipizia kisasi yeye mwenyewe. Mwenyezi Mungu atakapomletea bwana wangu mafanikio, umkumbuke mtumishi wako.”
32 Daudi akamwambia Abigaili, “Ahimidiwe Mwenyezi Mungu, Mungu wa Israeli, aliyekutuma kunilaki leo. 33 Ubarikiwe kwa uamuzi wako mzuri na kwa kunizuia nisimwage damu leo na kulipiza kisasi kwa mikono yangu. 34 La sivyo, hakika kama Mwenyezi Mungu, Mungu wa Israeli, aishivyo, ambaye amenizuia nisiwadhuru, kama usingekuja haraka kunilaki, hakuna mwanaume hata mmoja wa Nabali angeachwa hai kufikia mapambazuko.”
35 Ndipo Daudi akapokea kutoka mkononi mwake kile alichokuwa amemletea, naye akasema, “Nenda nyumbani mwako kwa amani; nimesikia maneno yako na kukujalia ombi lako.”
36 Abigaili alipoenda kwa Nabali, alikuwa ndani ya nyumba yake akifanya karamu kama ile ya mfalme. Naye alikuwa ana furaha nyingi, akiwa amelewa sana. Kwa hiyo Abigaili hakumwambia mumewe kitu chochote hadi asubuhi yake. 37 Basi asubuhi, ulevi ulipokuwa umemtoka Nabali, mkewe akamwambia mambo yote, nao moyo wake ukazimia, akawa kama jiwe. 38 Baada ya siku kumi, Mwenyezi Mungu akampiga Nabali, naye akafa.
39 Daudi aliposikia kwamba Nabali amekufa, akasema, “Ahimidiwe Mwenyezi Mungu, ambaye amenitetea dhidi ya Nabali kwa kuwa alinitendea kwa dharau. Amemzuia mtumishi wake asitende mabaya na Mwenyezi Mungu ameuleta ubaya wa Nabali juu ya kichwa chake mwenyewe.”
Kisha Daudi akatuma ujumbe kwa Abigaili kumwomba awe mke wake. 40 Watumishi wa Daudi wakaenda Karmeli na kumwambia Abigaili, wakisema, “Daudi ametutuma kwako kukuchukua uwe mkewe.”
41 Akasujudu uso wake ukielekea chini, akasema, “Mjakazi wako yuko hapa, tayari kuwatumikia na kuwanawisha miguu watumishi wa bwana wangu.” 42 Abigaili akainuka kwa haraka, akapanda punda wake, akihudumiwa na wajakazi wake watano, akaenda pamoja na wajumbe wa Daudi, naye akawa mkewe. 43 Pia Daudi alikuwa amemwoa Ahinoamu wa Yezreeli, wote wawili wakawa wake zake. 44 Lakini Sauli alikuwa amemwoza Mikali binti yake, aliyekuwa mkewe Daudi, kwa Palti mwana wa Laishi, kutoka Galimu.