17
Yehoshafati mfalme wa Yuda
Yehoshafati mwanawe akawa mfalme baada yake na akajiimarisha dhidi ya Israeli. Akaweka jeshi katika miji yote ya Yuda yenye ngome, na kuweka askari walinzi katika Yuda na katika miji ya Efraimu ambayo baba yake Asa alikuwa ameiteka.
Mwenyezi Mungu alikuwa na Yehoshafati kwa sababu katika miaka yake ya mwanzoni alienenda katika njia za Daudi baba yake. Hakutafuta Mabaali bali alimtafuta Mungu wa baba yake na kuzifuata amri zake badala ya kufuata desturi za Waisraeli. Kwa hiyo Mwenyezi Mungu akauimarisha ufalme chini ya uongozi wake, nao Yuda wote wakamletea Yehoshafati zawadi, hivyo akawa na utajiri mwingi na heshima. Moyo wake ukawa hodari katika njia za Mwenyezi Mungu na zaidi ya yote, akaondoa mahali pa juu pa kuabudia na nguzo za Maashera katika Yuda.
Katika mwaka wa tatu wa utawala wake Yehoshafati, alituma maafisa wake ambao ni Ben-Haili, Obadia, Zekaria, Nethaneli na Mikaya ili kufundisha katika miji ya Yuda. Pamoja nao walikuwa na Walawi kadhaa: Shemaya, Nethania, Zebadia, Asaheli, Shemiramothi, Yehonathani, Adoniya, Tobia, Tob-Adonia; na pamoja nao makuhani Elishama na Yehoramu. Wakafundisha Yuda yote, wakiwa wamechukua Kitabu cha Torati ya Mwenyezi Mungu; wakazunguka miji yote ya Yuda na kufundisha watu.
10 Kicho cha Mwenyezi Mungu kikawa juu ya falme zote za nchi zilizozunguka Yuda, hivyo hawakufanya vita na Yehoshafati. 11 Baadhi ya Wafilisti wakamletea Yehoshafati zawadi na fedha kama ushuru, nao Waarabu wakamletea mifugo: kondoo dume elfu saba na mia saba, na mbuzi elfu saba na mia saba.
12 Yehoshafati akaendelea kupata nguvu zaidi na zaidi, akajenga ngome na miji ya hazina katika Yuda, 13 na akawa na vifaa vingi katika miji ya Yuda. Pia aliweka wapiganaji wenye uzoefu huko Yerusalemu. 14 Wakaandikishwa katika jamaa zao kama ifuatavyo:
 
Kutoka Yuda, majemadari wa vikosi vya elfu:
Jemadari Adna akiwa na wapiganaji elfu mia tatu;
15 aliyefuata ni jemadari Yehohanani, akiwa na wapiganaji elfu mia mbili na themanini;
16 aliyefuata ni Amasia mwana wa Zikri, ambaye alijitolea kwa ajili ya kazi ya Mwenyezi Mungu, akiwa na wapiganaji elfu mia mbili.
17 Kutoka Benyamini:
Eliada, mpiganaji hodari, akiwa na watu elfu mia mbili wenye nyuta na ngao;
18 aliyefuata ni Yehozabadi, akiwa na wapiganaji elfu mia moja na themanini tayari kwa vita.
 
19 Hawa ndio wapiganaji waliomtumikia mfalme, mbali na ambao mfalme aliwaweka katika miji yenye ngome katika Yuda yote.