13
Maonyo ya mwisho
1 Hii itakuwa mara ya tatu mimi kuja kwenu. “Shtaka lolote lazima lithibitishwe na mashahidi wawili au watatu.” 2 Niliwaonya nilipokuwa pamoja nanyi mara ya pili. Sasa narudia wakati sipo, kwamba nikija tena sitawahurumia wale waliokuwa wametenda dhambi hapo awali au wengine wote, 3 kwa kuwa mnadai uthibitisho kwamba Al-Masihi anazungumza kwa kunitumia mimi. Yeye si dhaifu katika kushughulika nanyi, bali ana nguvu kati yenu. 4 Kwa kuwa alisulubiwa katika udhaifu, lakini anaishi kwa nguvu za Mungu. Vivyo hivyo, sisi tu dhaifu kupitia kwake, lakini katika kuwashughulikia ninyi tutaishi pamoja naye kwa nguvu za Mungu.
5 Jichunguzeni wenyewe mwone kama mnaishi katika imani. Jipimeni wenyewe. Je, hamtambui ya kuwa Isa Al-Masihi yu ndani yenu? Kama sivyo, basi, mmeshindwa kufikia kipimo hicho! 6 Natumaini mtaona kuwa sisi hatukushindwa. 7 Lakini tunamwomba Mungu msije mkatenda kosa lolote, si ili sisi tuonekane kuwa tumeshinda hilo jaribio, bali ili ninyi mtende lililo haki, hata kama tutaonekana kuwa tumeshindwa. 8 Kwa maana hatuwezi kufanya lolote kinyume na kweli, bali kuithibitisha kweli tu. 9 Tunafurahi wakati wowote tunapokuwa dhaifu, lakini ninyi mkawa na nguvu. Nayo maombi yetu ni kwamba mpate kuwa wakamilifu. 10 Hii ndiyo sababu nawaandikia mambo haya wakati sipo, ili nikija nisiwe mkali katika kutumia mamlaka yangu, mamlaka Bwana Isa aliyonipa ya kuwajenga ninyi wala si ya kuwabomoa.
Salamu za mwisho
11 Hatimaye, ndugu zangu, kwaherini. Kuweni wakamilifu, farijianeni, kuweni na nia moja, na mkae kwa amani. Naye Mungu wa upendo na amani atakuwa pamoja nanyi.
12 Salimianeni kwa busu takatifu.
13 Watakatifu wote wanawasalimu.
14 Neema ya Bwana Isa Al-Masihi, na upendo wa Mungu, na ushirika wa Roho wa Mungu ukae nanyi nyote.