11
Mpende na umtii Mwenyezi Mungu
1 Mpende Mwenyezi Mungu, Mungu wako, na kushika masharti yake, amri zake, sheria zake na maagizo yake siku zote. 2 Kumbuka hivi leo kwamba sio watoto wako walioona na kujua adhabu ya Mwenyezi Mungu, Mungu wako: utukufu wake, mkono wake wenye nguvu, mkono wake ulionyooshwa; 3 ishara alizozifanya na mambo aliyoyafanya katikati ya Misri, kwa Farao mfalme wa Misri na kwa nchi yake yote; 4 lile alilolifanyia jeshi la Wamisri, farasi na magari yake ya vita, jinsi alivyowafurikisha na maji ya Bahari ya Shamu walipokuwa wakiwafuatilia ninyi, na jinsi Mwenyezi Mungu alivyowaletea angamizi la kudumu juu yao. 5 Sio watoto wenu walioyaona yale Mungu aliyowafanyia huko jangwani hadi mkafika mahali hapa, 6 wala lile Mungu alilowafanyia Dathani na Abiramu, wana wa Eliabu wa kabila la Reubeni, wakati ardhi ilipofungua kinywa chake katikati ya Israeli yote, ikawameza pamoja na walio nyumbani mwao, mahema yao na kila kitu hai kilichokuwa mali yao. 7 Bali ni macho yenu wenyewe yaliyoyaona mambo haya yote makuu Mwenyezi Mungu aliyoyatenda.
8 Kwa hiyo fuateni maagizo yote ninayowapa leo, ili mpate kuwa na nguvu za kuingia na kuiteka nchi ambayo mnavuka Yordani kuimiliki, 9 ili mpate kuishi siku nyingi katika nchi ambayo Mwenyezi Mungu aliapa kuwapa baba zenu na wazao wao, nchi inayotiririka maziwa na asali. 10 Nchi mnayoiingia kuimiliki haifanani na nchi ya Misri mlikotoka, ambako mlipanda mbegu zenu na kunyunyizia maji kwa miguu kama bustani ya mboga. 11 Lakini nchi mnayovuka Yordani kuimiliki ni nchi ya milima na mabonde inayokunywa maji ya mvua ya mbinguni. 12 Ni nchi ambayo Mwenyezi Mungu, Mungu wenu, anaitunza; macho ya Mwenyezi Mungu, Mungu wenu, yanaitazama daima kutoka mwanzo wa mwaka hadi mwisho wa mwaka.
13 Hivyo mkiyatii maagizo yangu ninayowapa leo kwa uaminifu, yaani kwa kumpenda Mwenyezi Mungu, Mungu wenu, na kumtumikia kwa moyo wako wote na kwa roho yenu yote, 14 ndipo atawanyeshea mvua katika nchi yenu kwa majira yake, mvua ya masika na ya vuli, ili mpate kuvuna nafaka zenu, divai mpya na mafuta. 15 Nitawapa majani katika malisho yako kwa ajili ya ng’ombe wenu, nanyi mtakula na kushiba.
16 Jihadharini, la sivyo mtashawishika kugeuka na kuabudu miungu mingine na kuisujudia. 17 Ndipo hasira ya Mwenyezi Mungu itawaka dhidi yenu, naye atafunga mbingu ili mvua isinyeshe nayo ardhi haitatoa mazao, nanyi mtaangamia upesi katika nchi nzuri ambayo Mwenyezi Mungu anawapa. 18 Yawekeni haya maneno yangu katika mioyo yenu na akili zenu, yafungeni kama alama juu ya mikono yenu na kwenye paji za nyuso zenu. 19 Wafundisheni watoto wenu, yazungumzeni mnapoketi nyumbani na mnapotembea njiani, mnapolala na mnapoamka. 20 Yaandikeni juu ya miimo ya nyumba zenu na juu ya malango yenu, 21 ili siku zenu na siku za watoto wenu zipate kuwa nyingi katika nchi ile Mwenyezi Mungu aliyoapa kuwapa baba zenu, kama zilivyo nyingi siku za mbingu juu ya nchi.
22 Mkizingatia kwa makini maagizo haya yote ninayowapa kuyafuata, ya kumpenda Mwenyezi Mungu, Mungu wenu, kuenenda katika njia zake zote na kushikamana naye kwa uthabiti, 23 ndipo Mwenyezi Mungu atawafukuza mataifa haya yote mbele yako, nawe utawafukuza mataifa yaliyo makubwa na yenye nguvu kuliko wewe. 24 Kila mahali mtakapoweka mguu wenu patakuwa penu: Nchi yenu itaenea kutoka jangwa la Lebanoni, na kutoka Mto Frati hadi bahari ya magharibi*yaani Bahari ya Mediterania. 25 Hapatakuwa na mtu atakayeweza kusimama dhidi yenu. Mwenyezi Mungu, Mungu wenu, kama alivyoahidi, ataweka juu ya nchi yote utisho na hofu kwa ajili yenu popote mtaenda.
26 Tazama, leo ninaweka mbele yenu baraka na laana: 27 baraka kama mtatii maagizo ya Mwenyezi Mungu, Mungu wenu, ninayowapa leo; 28 laana kama hamtatii maagizo ya Mwenyezi Mungu, Mungu wenu, na kuacha njia ninayowaamuru leo kwa kufuata miungu mingine, ambayo hamkuijua. 29 Mwenyezi Mungu, Mungu wenu, atakapokuwa amewaleta katika nchi mnayoiingia kuimiliki, mtatangaza baraka kutoka Mlima Gerizimu, na kutangaza laana kutoka Mlima Ebali. 30 Kama mnavyofahamu, milima hii ipo ng’ambo ya Yordani, magharibi mwa barabara, kuelekea machweo ya jua, karibu na mialoni ya More, katika nchi ya wale Wakanaani wanaoishi Araba, jirani na Gilgali. 31 Karibu mvuke ng’ambo ya Yordani kuingia na kuimiliki nchi ambayo Mwenyezi Mungu, Mungu wenu, anawapa. Mtakapokuwa mmeimiliki na mnaishi humo, 32 hakikisheni kwamba mnatii amri na sheria zote ninazoziweka mbele yenu leo.