12
Pasaka na pigo la mwisho
Mwenyezi Mungu akamwambia Musa na Haruni katika nchi ya Misri, “Mwezi huu utakuwa mwanzo wa miezi kwenu, yaani mwezi wa kwanza wa mwaka wenu. Iambie jumuiya yote ya Israeli kwamba katika siku ya kumi ya mwezi huu, kila mtu atatwaa mwana-kondoo mmoja kwa ajili ya jamaa yake, mmoja kwa kila nyumba. Ikiwa nyumba yoyote ina watu wachache wasioweza kumaliza huyo mwana-kondoo mzima, nyumba hiyo itabidi ishirikiane na nyumba ya jirani wa karibu, baada ya kuzingatia idadi ya watu waliomo. Mtaangalia ni kiasi gani cha nyama kitahitajika kulingana na mahitaji ya kila mtu. Wanyama mtakaowachagua, lazima wawe wa kiume wa umri wa mwaka mmoja wasiokuwa na dosari, mwaweza kuwachukua kati ya kondoo au mbuzi. Tunzeni wanyama hao hadi siku ya kumi na nne ya mwezi, ambapo lazima watu wa jumuiya yote ya Israeli wachinje wanyama hao wakati wa jioni. Ndipo watakapochukua sehemu ya hiyo damu na kuipaka kwenye vizingiti vya juu, na miimo ya milango ya nyumba ambamo watakula wana-kondoo hao. Usiku huo huo watakula nyama iliyookwa kwenye moto, pamoja na mboga chungu za majani na mikate isiyotiwa chachu. Msile nyama mbichi wala iliyochemshwa, lakini iwe imeokwa kwenye moto, kichwa, miguu na nyama zake za ndani. 10 Msibakize nyama yoyote hadi asubuhi; nazo kama zitabakia hadi asubuhi, lazima mziteketeze kwa moto. 11 Hivi ndivyo mtakavyokula: Mtajifunga mikanda viunoni, mtakuwa mmevaa viatu vyenu miguuni na kushika fimbo zenu mkononi mwenu. Mle kwa haraka; hii ni Pasaka*Sherehe iliyowakumbusha Waisraeli jinsi Mwenyezi Mungu alivyowakomboa kutoka utumwani huko Misri. ya Mwenyezi Mungu.
12 “Usiku huo huo nitapita katika nchi yote ya Misri na kumuua kila mzaliwa wa kwanza, wa wanadamu na wa wanyama, nami nitaihukumu miungu yote ya Misri. Mimi ndimi Mwenyezi Mungu. 13 Damu itakuwa ishara kwa ajili yenu ya kuonesha nyumba ambazo mtakuwamo; nami nitakapoiona damu, nitapita juu yenu. Hakuna pigo la uharibifu litakalowagusa ninyi nitakapoipiga Misri.
14 “Siku hii itakuwa kumbukumbu kwenu, mtaiadhimisha kuwa sikukuu kwa Mwenyezi Mungu, katika vizazi vyenu vyote: mtalishika kuwa agizo la kudumu. 15 Kwa siku saba mtakula mikate isiyotiwa chachu. Katika siku ya kwanza mtaondoa chachu yote ndani ya nyumba zenu, kwa maana yeyote atakayekula chochote chenye chachu kuanzia siku ya kwanza hadi ya saba lazima akatiliwe mbali kutoka Israeli. 16 Katika siku ya kwanza mtakuwa na kusanyiko takatifu, na kusanyiko jingine katika siku ya saba. Katika siku hizo msifanye kazi kamwe isipokuwa kutayarisha chakula cha kila mmoja; hilo ndilo tu mtakalofanya.
17 “Mtaadhimisha Sikukuu ya Mikate Isiyotiwa Chachu, kwa sababu hiyo ndiyo siku ile niliyovitoa vikosi vyenu kutoka Misri. Mtaiadhimisha siku hii kwa vizazi vyenu vyote kuwa agizo la kudumu. 18 Katika mwezi wa kwanza mtakula mikate isiyotiwa chachu, kuanzia jioni ya siku ya kumi na nne hadi jioni ya siku ya ishirini na moja. 19 Kwa muda wa siku saba isionekane chachu yoyote katika nyumba zenu. Yeyote alaye chochote chenye chachu ndani yake, lazima akatiliwe mbali kutoka jumuiya ya Israeli, akiwa ni mgeni au mzawa. 20 Msile chochote kilichotiwa chachu. Popote mnapoishi, ni lazima mle mikate isiyotiwa chachu.”
21 Ndipo Musa akawaita wazee wote wa Israeli na kuwaambia, “Nendeni mara moja mkachague wanyama kwa ajili ya jamaa zenu, mkachinje mwana-kondoo wa Pasaka. 22 Chukueni kitawi cha hisopo, mkichovye kwenye damu iliyopo kwenye sinia, na kuipaka sehemu ya hiyo damu kwenye vizingiti, na kwenye miimo yote miwili ya milango. Mtu yeyote asitoke nje ya mlango wa nyumba yake hadi asubuhi. 23 Mwenyezi Mungu apitapo katika nchi yote kuwapiga Wamisri, ataiona damu juu ya vizingiti na kwenye miimo ya milango, naye atapita juu, wala hatamruhusu mwangamizi kuingia katika nyumba zenu na kuwapiga ninyi.
24 “Shikeni maagizo haya yawe kanuni ya kudumu kwenu na kwa ajili ya wazao wenu. 25 Mtakapoingia katika nchi Mwenyezi Mungu atakayowapa kama alivyoahidi, shikeni desturi hii. 26 Watoto wenu watakapowauliza, ‘Sikukuu hii ina maana gani kwenu?’ 27 Basi waambieni, ‘Hii ni dhabihu ya Pasaka kwa Mwenyezi Mungu, ambaye alipita juu ya nyumba za Waisraeli katika nchi ya Misri, na hakudhuru nyumba zetu alipowapiga Wamisri.’ ” Ndipo Waisraeli walisujudu na kuabudu. 28 Waisraeli wakafanya kama vile Mwenyezi Mungu alivyomwagiza Musa na Haruni.
29 Ilipofika usiku wa manane, Mwenyezi Mungu akawapiga wazaliwa wa kwanza wote katika Misri, kuanzia mzaliwa wa kwanza wa Farao, mrithi wa kiti cha ufalme, hadi mzaliwa wa kwanza wa mfungwa, aliyekuwa gerezani, na wazaliwa wa kwanza wa mifugo yote pia. 30 Farao, na maafisa wake wote, na Wamisri wote wakaamka usiku, na kulikuwa na kilio kikubwa katika nchi ya Misri, kwa kuwa hapakuwa nyumba hata moja ambayo hakufa mtu.
Kutoka
31 Wakati huo Farao akawaita Musa na Haruni na kuwaambia, “Ondokeni! Tokeni kwa watu wangu, ninyi pamoja na Waisraeli! Nendeni mkamwabudu Mwenyezi Mungu kama mlivyoomba. 32 Chukueni makundi yenu ya kondoo na mbuzi pamoja na ng’ombe, kama mlivyosema, nanyi mwende zenu. Nanyi pia mnibariki.”
33 Wamisri wakawahimiza Waisraeli waondoke kwa haraka na kuacha nchi yao. Kwa kuwa walisema, “La sivyo, tutakufa wote!” 34 Hivyo watu wakachukua donge lao la unga kabla ya kutiwa chachu, wakaweka ndani ya mabakuli ya kukandia, wakayaviringisha katika mavazi na kuyabeba mabegani mwao. 35 Waisraeli wakafanya kama Musa alivyowaelekeza, nao wakawaomba Wamisri wawapatie vitu vya fedha, dhahabu na mavazi. 36 Basi Mwenyezi Mungu alikuwa amewafanya Wamisri kuwa wakarimu kwa hawa watu, wakawapatia Waisraeli vile walivyotaka kwao; kwa hiyo wakawateka nyara Wamisri.
37 Waisraeli wakasafiri kutoka Ramesesi hadi Sukothi. Walikuwa wanaume wapatao elfu mia sita waliotembea kwa miguu, bila kuhesabu wanawake na watoto. 38 Watu wengine wengi wakafuatana nao, pamoja na makundi makubwa ya mifugo, wakiwemo kondoo, mbuzi na ng’ombe. 39 Wakatengeneza maandazi yasiyotiwa chachu kwa ule unga uliokandwa waliokuwa wameutoa Misri, donge hilo la unga halikuwa limetiwa chachu, kwa kuwa walikuwa wameondolewa Misri kwa haraka nao hawakuwa na muda wa kujiandalia chakula.
40 Waisraeli waliishi Misri kwa muda wa miaka mia nne na thelathini (430). 41 Siku ya mwisho ya hiyo miaka mia nne na thelathini (430), vikosi vyote vya Mwenyezi Mungu viliondoka Misri. 42 Kwa sababu Mwenyezi Mungu aliutenga usiku ule ili kuwatoa Waisraeli katika nchi ya Misri, basi Waisraeli wote wanapaswa kuadhimisha usiku huu kwa kukesha ili kumheshimu Mwenyezi Mungu katika vizazi vijavyo.
Masharti kwa ajili ya Pasaka
43 Mwenyezi Mungu akawaambia Musa na Haruni, “Haya ndio masharti kwa ajili ya Pasaka:
“Mgeni hataruhusiwa kula Pasaka. 44 Mtumwa yeyote ambaye mmemnunua aweza kuila kama mmemtahiri, 45 lakini kibarua yeyote au msafiri haruhusiwi kula.
46 “Sharti iliwe ndani ya nyumba; msichukue nyama yoyote nje ya nyumba hiyo. Msiuvunje mfupa wowote. 47 Jumuiya yote ya Israeli ni lazima waiadhimishe Pasaka hiyo.
48 “Mgeni aishiye miongoni mwenu ambaye anataka kuadhimisha Pasaka ya Mwenyezi Mungu ni lazima wanaume wote waliomo nyumbani mwake wawe wametahiriwa, ndipo aweze kushiriki kama mzawa. Mwanaume yeyote asiyetahiriwa haruhusiwi kuila. 49 Sheria hiyo hiyo itamuhusu mzawa na mgeni anayeishi miongoni mwenu.”
50 Waisraeli wote walifanya kama vile Mwenyezi Mungu alivyomwagiza Musa na Haruni. 51 Siku ile ile Mwenyezi Mungu akawatoa Waisraeli katika nchi ya Misri kwa vikosi vyao.

*12:11 Sherehe iliyowakumbusha Waisraeli jinsi Mwenyezi Mungu alivyowakomboa kutoka utumwani huko Misri.