2
Wito wa Ezekieli
1 Akaniambia, “Mwanadamu, simama kwa miguu yako nami nitasema nawe.” 2 Alipokuwa akiongea nami, Roho wa Mungu akanijia na kunisimamisha wima, nikamsikia akisema nami.
3 Akaniambia: “Mwanadamu, ninakutuma kwa Waisraeli, taifa ambalo limeniasi mimi; wao na baba zao wameniasi hadi leo. 4 Watu ninaokutuma kwao ni wakaidi na wabishi. Waambie, ‘Hivi ndivyo asemavyo Bwana Mungu Mwenyezi.’ 5 Kama watasikiliza au hawatasikiliza, kwa kuwa wao ni nyumba ya uasi, watajua nabii amekuwa miongoni mwao. 6 Nawe mwanadamu, usiwaogope wao wala maneno yao. Usiogope, ijapo michongoma na miiba vinakuzunguka na unaishi katikati ya nge. Usiogope yale wasemayo wala usitishwe nao, ijapo wao ni nyumba ya uasi. 7 Lazima uwaambie maneno yangu, ikiwa watasikiliza au hawatasikiliza, kwa kuwa wao ni waasi. 8 Lakini wewe mwanadamu, sikiliza ninalokuambia. Usiasi kama hiyo nyumba ya uasi. Fungua kinywa chako na ule nikupacho.”
9 Ndipo nikatazama, nami nikaona mkono ulionyooshwa kunielekea. Nao ulikuwa na kitabu, 10 ambacho alikikunjua mbele yangu. Pande zote mbili kilikuwa kimeandikwa maneno ya maombolezo, na vilio na ole.