28
Yakobo akimbilia kwa Labani
1 Basi Isaka akamwita Yakobo, akambariki na akamwamuru, akisema, “Usioe mwanamke Mkanaani. 2 Nenda mara moja hadi Padan-Aramu, kwenye nyumba ya Bethueli, baba wa mama yako. Uchukue mke kati ya binti za Labani ambaye ni ndugu wa mama yako. 3 Mungu Mwenyezi*Kiebrania El-Shaddai (yaani Mungu Mwenye utoshelevu wote). na akubariki, uwe na uzao, uongezeke idadi yako hadi upate kuwa jamii kubwa ya watu. 4 Akupe wewe na uzao wako baraka aliyopewa Ibrahimu, upate kumiliki nchi unayoishi sasa kama mgeni, nchi ambayo Mungu alimpa Ibrahimu.” 5 Kisha Isaka akamuaga Yakobo, naye akaenda Padan-Aramu, kwa Labani mwana wa Bethueli Mwaramu†au Mshami, ndugu wa Rebeka, mama yao Yakobo na Esau.
6 Basi Esau akajua kuwa Isaka amembariki Yakobo na kumtuma Padan-Aramu ili achukue mke huko, na kwamba alipombariki alimwamuru, akisema, “Usioe mke katika binti za Wakanaani,” 7 tena kwamba Yakobo amewatii baba yake na mama yake, naye ameenda Padan-Aramu. 8 Esau akatambua jinsi baba yake Isaka alivyowachukia binti za Wakanaani. 9 Ndipo Esau akaenda kwa Ishmaeli, akamwoa Mahalati, ndugu wa Nebayothi na binti ya Ishmaeli mwana wa Ibrahimu, kuongezea wale wake wengine aliokuwa nao.
Ndoto ya Yakobo huko Betheli
10 Yakobo akatoka Beer-Sheba kwenda Harani. 11 Alipofika mahali fulani, akalala hapo kwa sababu jua lilikuwa limetua. Akachukua jiwe moja la mahali pale, akaliweka chini ya kichwa chake, akajinyoosha na akalala usingizi. 12 Akaota ndoto, na katika ndoto hiyo aliona ngazi imesimamishwa juu ya ardhi, ncha yake ikiwa imefika mbinguni. Nao malaika wa Mungu walikuwa wakipanda na kushuka kwa ngazi hiyo. 13 Juu yake alisimama Mwenyezi Mungu, akasema, “Mimi ni Mwenyezi Mungu, Mungu wa baba yako Ibrahimu, na Mungu wa Isaka. Nchi ambayo umelala juu yake, nitakupa wewe na uzao wako. 14 Uzao wako utakuwa kama mavumbi ya nchi, nawe utaenea upande wa magharibi na mashariki, kaskazini na kusini. Kupitia wewe na uzao wako, mataifa yote ya duniani yatabarikiwa. 15 Niko pamoja nawe, nami nitakulinda popote utakapoenda, na nitakurudisha katika nchi hii. Sitakuacha hadi nitakapofanya hayo niliyokuahidi.”
16 Yakobo alipoamka kutoka usingizi, akawaza, “Hakika Mwenyezi Mungu yuko mahali hapa, wala mimi sikujua.” 17 Kwa hiyo akaogopa, akasema, “Mahali hapa panatisha kama nini! Bila shaka hapa ndipo nyumba ya Mungu ilipo; hili ni lango la mbinguni.”
18 Kesho yake asubuhi na mapema, Yakobo akalichukua lile jiwe aliloliweka chini ya kichwa chake, akalisimamisha kama nguzo, na kumimina mafuta juu yake. 19 Mahali pale akapaita Betheli‡maana yake Nyumba ya Mungu, ingawa mji ule hapo awali uliitwa Luzu.
20 Kisha Yakobo akaweka nadhiri, akisema, “Mungu akiwa pamoja nami na kunilinda katika safari hii, akinipa chakula nile na nguo nivae, 21 na nirudi salama nyumbani mwa baba yangu, hapo ndipo Mwenyezi Mungu atakuwa Mungu wangu. 22 Nalo jiwe hili nililolisimamisha kama nguzo litakuwa nyumba ya Mungu, na katika yote utakayonipa nitakutolea sehemu ya kumi.”