2
Wokovu mkuu
1 Kwa hiyo, imetupasa kuwa waangalifu sana kuhusu kile tulichosikia, ili tusije tukakiacha. 2 Kwa kuwa kama ujumbe ulionenwa na malaika ulikuwa imara, na kila uasi na kutokutii kulipata adhabu ya haki, 3 je, sisi tutapataje kupona kama tusipojali wokovu mkuu namna hii? Wokovu huu, ambao mwanzo ulitangazwa na Bwana Isa, ulithibitishwa kwetu na wale waliomsikia. 4 Pia Mungu aliushuhudia kwa ishara, maajabu, na kwa miujiza mbalimbali, na karama za Roho wa Mungu alizozigawa kulingana na mapenzi yake.
Isa alifananishwa na ndugu zake
5 Mungu hakuuweka ulimwengu ujao ambao tunanena habari zake chini ya malaika. 6 Lakini kuna mahali mtu mmoja ameshuhudia, akisema:
“Mwanadamu ni kitu gani hata unamfikiria,
binadamu ni nani hata unamjali?
7 Umemfanya chini kidogo kuliko malaika;
ukamvika taji la utukufu na heshima,
8 nawe umeweka vitu vyote chini ya miguu yake.”
Kwa kuweka vitu vyote chini yake, Mungu hakuacha kitu chochote ambacho hakukiweka chini ya mwanadamu. Lakini kwa sasa, hatuoni kwamba kila kitu kiko chini yake. 9 Lakini twamwona Isa, aliyefanywa chini kidogo kuliko malaika, sasa akiwa amevikwa taji la utukufu na heshima kwa sababu alistahimili mauti, ili kwa neema ya Mungu apate kuonja mauti kwa ajili ya kila mtu.
10 Ili kuwaleta wana wengi katika utukufu, ilifaa kwamba Mungu, ambaye ni kwa ajili yake na kupitia kwake kila kitu kimekuwepo, amkamilishe mwanzilishi wa wokovu wao kupitia kwa mateso yake. 11 Yeye awafanyaye watu kuwa watakatifu, pamoja na hao ambao hufanywa watakatifu, wote hutoka katika jamaa moja. Hivyo Isa haoni aibu kuwaita ndugu zake. 12 Yeye anasema,
“Nitalitangaza jina lako kwa ndugu zangu;
mbele ya kusanyiko nitaimba sifa zako.”
13 Tena,
“Nitaweka tumaini langu kwake.”
Tena anasema,
“Niko hapa, pamoja na watoto ambao Mungu amenipa.”
14 Basi kwa kuwa watoto wana mwili na damu, yeye pia alishiriki katika ubinadamu wao, ili kwa kifo chake, apate kumwangamiza huyo mwenye nguvu za mauti, yaani ibilisi, 15 na kuwaweka huru wale waliokuwa utumwani maisha yao yote kwa sababu ya kuogopa mauti. 16 Kwa kuwa ni dhahiri kwamba hakuja kusaidia malaika, bali uzao wa Ibrahimu. 17 Kwa sababu hii ilibidi afanane na ndugu zake kwa kila hali, ili apate kuwa Kuhani Mkuu mwenye huruma na mwaminifu katika kumtumikia Mungu, ili pia apate kufanya upatanisho kwa ajili ya dhambi za watu. 18 Kwa kuwa yeye mwenyewe aliteswa alipojaribiwa, aweza kuwasaidia wale wanaojaribiwa.