20
Unabii dhidi ya Misri na Kushi
1 Mwaka ule jemadari mkuu alitumwa na Mfalme Sargoni wa Ashuru, naye akaja Ashdodi, akaushambulia na kuuteka, 2 wakati huo Mwenyezi Mungu alisema kwa kinywa cha Isaya mwana wa Amozi. Akamwambia, “Vua gunia kutoka mwilini mwako na viatu kutoka miguuni mwako.” Naye akafanya hivyo, akitembea uchi, bila viatu.
3 Kisha Mwenyezi Mungu akasema, “Kama mtumishi wangu Isaya alivyotembea uchi na bila viatu kwa miaka mitatu, kama ishara na dalili mbaya dhidi ya nchi ya Misri na Kushi, 4 vivyo hivyo mfalme wa Ashuru atawaongoza mateka wa Wamisri, na watu wa uhamisho wa Kushi, uchi na bila viatu, vijana hata wazee, wakiwa matako wazi, kwa aibu ya Wamisri. 5 Wale waliotegemea Kushi na kujivunia Misri wataogopa na kuaibika. 6 Katika siku ile watu wanaoishi katika pwani hii watasema, ‘Tazama lililowapata wale tuliowategemea, wale tuliowakimbilia kwa msaada na wokovu kutoka mikononi mwa mfalme wa Ashuru! Tutawezaje basi kupona?’ ”