16
Mgawo kwa Efraimu na Manase
1 Mgawanyo wa Yusufu ulianzia Yordani ya Yeriko, mashariki mwa miji ya Yeriko na kutoka hapo ulipanda kupitia jangwani na kuingia katika nchi ya vilima ya Betheli. 2 Ukaendelea kutoka Betheli (ndiyo Luzu), ukavuka kuingia eneo la Waarki huko Atarothi, 3 ukateremkia kuelekea magharibi hadi eneo la Wayafleti ukienea hadi eneo la Beth-Horoni ya Chini hadi Gezeri, ukiishia baharini.
4 Kwa hiyo Manase na Efraimu, wazao wa Yusufu, walipokea urithi wao.
5 Hili ndilo lilikuwa eneo la Efraimu, kufuatana na koo zao:
Mpaka wa urithi wao ulianzia Ataroth-Adari upande wa mashariki hadi Beth-Horoni ya Juu, 6 na kuendelea mpaka baharini. Kutoka Mikmeta upande wa kaskazini ulipinda kuelekea mashariki hadi Taanath-Shilo, ukiupita hadi Yanoa upande wa mashariki. 7 Kisha uliteremka kutoka Yanoa hadi Atarothi na Naara, ukagusa Yeriko na kutokea katika Mto Yordani. 8 Kutoka Tapua, mpaka ulienda magharibi hadi Bonde la Kana na kuishia baharini. Huu ulikuwa ndio urithi wa kabila la Waefraimu, kufuatana na koo zao.
9 Pia ulijumuisha miji yote na vijiji vyake ambavyo vilitengwa kwa ajili ya Waefraimu ndani ya urithi wa kabila la Manase.
10 Hawakuwatoa Wakanaani walioishi Gezeri; hadi leo Wakanaani wanaishi miongoni mwa watu wa Efraimu, lakini wanatumikishwa kwa kazi ngumu.