17
Mgawo wa nusu nyingine ya Manase upande wa magharibi
Huu ndio mgawo wa kabila la Manase, mzaliwa wa kwanza wa Yusufu. Makiri, mzaliwa wa kwanza wa Manase, aliyekuwa baba wa Wagileadi, alipewa Gileadi na Bashani kwa sababu alikuwa hodari katika vita. Kwa hiyo mgawo huu ulikuwa kwa ajili ya watu wa Manase waliokuwa wamebaki, ambao ni koo za Abiezeri, Heleki, Asirieli, Shekemu, Heferi na Shemida. Hawa ndio wanaume wale wengine wa uzao wa Manase mwana wa Yusufu kwa koo zao.
Basi Selofehadi mwana wa Heferi, mwana wa Gileadi, mwana wa Makiri, mwana wa Manase hakuwa na wana wa kiume ila binti tu, ambao majina yao yalikuwa Mahla, Noa, Hogla, Milka na Tirsa. Wakamwendea kuhani Eleazari, Yoshua mwana wa Nuni, na viongozi, wakasema: “Mwenyezi Mungu alimwagiza Musa atupatie urithi miongoni mwa ndugu zetu.” Kwa hiyo Yoshua akawapa urithi pamoja na ndugu wa baba yao, kufuatana na agizo la Mwenyezi Mungu. Zaidi ya Gileadi na Bashani mashariki mwa Yordani, fungu la Manase lilikuwa na sehemu kumi za nchi, kwa sababu wale binti za kabila la Manase walipokea urithi pamoja na wana wa kiume. Nchi ya Gileadi ilikuwa mali ya wazao wa Manase waliobaki.
Eneo la Manase lilienea kuanzia Asheri hadi Mikmeta mashariki mwa Shekemu. Mpaka ule ulielekea upande wa kusini kutoka pale kujumuisha watu walioishi En-Tapua. (Nchi ya Tapua ilikuwa mali ya Manase, lakini Tapua yenyewe iliyo mpakani mwa nchi ya Manase ilikuwa ya Waefraimu.) Kisha mpaka ule uliendelea kuelekea kusini hadi Bonde la Kana. Kulikuwa na miji ya Efraimu iliyokuwa miongoni mwa miji ya Manase, lakini mpaka wa Manase ulikuwa upande wa kaskazini wa lile bonde, na kuishia kwenye bahari. 10 Nchi ya kusini ilikuwa ya Efraimu, na ile iliyokuwa upande wa kaskazini ilikuwa ya Manase. Eneo la Manase lilifika bahari na likapakana na Asheri upande wa kaskazini, na Isakari upande wa mashariki.
11 Katika Isakari na Asheri Manase alikuwa na miji pia: Beth-Shani, Ibleamu na watu wa Dori, Endori, Taanaki na Megido, pamoja na makazi yote ya miji hiyo (ya tatu katika orodha ni Nafothi*yaani Nafoth-Dori).
 
12 Lakini Wamanase hawakuweza kuimiliki miji hii, kwa kuwa Wakanaani walikazana kuishi katika maeneo hayo. 13 Hata hivyo, Waisraeli walivyoendelea kupata nguvu waliwatumikisha Wakanaani na kuwatia katika kazi za kulazimishwa, lakini hawakuwafukuza kabisa.
14 Wana wa Yusufu wakamwambia Yoshua, “Kwa nini umetupatia sisi mgawo mmoja tu na sehemu moja tu kuwa urithi? Sisi tu watu wengi sana, na Mwenyezi Mungu ametubariki kwa wingi.”
15 Yoshua akajibu, “Kama ninyi ni wengi sana, na kama nchi ya vilima ya Efraimu ni ndogo sana kwenu, pandeni msituni mkafyeke eneo kwa ajili yenu wenyewe huko kwenye nchi ya Waperizi na Warefai.”
16 Wana wa Yusufu wakajibu, “Hiyo nchi ya vilima haitutoshi, nao Wakanaani wote wanaoishi katika tambarare wana magari ya vita ya chuma, yaani wale walio Beth-Shani na makazi yake, na wale walio katika Bonde la Yezreeli.”
17 Lakini Yoshua akanena na nyumba ya Yusufu, yaani Efraimu na Manase: “Ninyi ni wengi sana na wenye nguvu sana. Hamtakuwa na mgawo mmoja tu, 18 bali pia nchi hii ya vilima yenye msitu. Ifyekeni, nayo mipaka yake itakuwa yenu umbali mtakaoweza kufika. Ingawa Wakanaani wana magari ya vita ya chuma, na wana nguvu, mtaweza kuwafukuza humo.”

*17:11 yaani Nafoth-Dori