2
Sadaka ya nafaka
“ ‘Mtu yeyote aletapo sadaka ya nafaka kwa Mwenyezi Mungu, sadaka yake itakuwa ya unga laini. Atamimina mafuta juu yake, aweke uvumba juu yake, naye atapeleka kwa makuhani wana wa Haruni. Kuhani atachukua konzi moja unga laini na mafuta, pamoja na uvumba wote, na kuviteketeza kama sehemu ya kumbukumbu juu ya madhabahu, sadaka iliyotolewa kwa moto, harufu nzuri ya kumpendeza Mwenyezi Mungu. Sadaka ya nafaka iliyobaki ni ya Haruni na wanawe; ni sehemu ya sadaka iliyo takatifu sana iliyotolewa kwa Mwenyezi Mungu kwa moto.
“ ‘Kama utaleta sadaka ya nafaka iliyookwa, itakuwa ya unga laini: iwe maandazi yaliyotengenezwa bila kutiwa chachu, yaliyochanganywa na mafuta, au mikate myembamba iliyotengenezwa bila kutiwa chachu na iliyopakwa mafuta. Iwapo sadaka yako ya nafaka imeandaliwa kwenye kikaango, itakuwa ni ya unga laini uliochanganywa na mafuta, bila chachu. Vunjavunja na kumimina mafuta juu yake; hii ni sadaka ya nafaka. Ikiwa sadaka yako ya nafaka imepikwa kwenye sufuria, itatengenezwa kwa unga laini na mafuta. Ilete hiyo sadaka ya nafaka iliyotengenezwa kwa vitu hivi kwa Mwenyezi Mungu; mkabidhi kuhani, ambaye ataipeleka madhabahuni. Naye atatoa ile sehemu ya kumbukumbu katika hiyo sadaka ya nafaka, na kuiteketeza juu ya madhabahu kuwa sadaka iliyotolewa kwa moto, harufu nzuri ya kumpendeza Mwenyezi Mungu. 10 Sadaka ya nafaka iliyobaki ni ya Haruni na wanawe; ni sehemu ya sadaka takatifu sana kati ya sadaka zilizotolewa kwa Mwenyezi Mungu kwa moto.
11 “ ‘Kila sadaka ya nafaka unayoleta kwa Mwenyezi Mungu ni lazima ifanywe bila kutiwa chachu, kwa kuwa huna ruhusa kuchoma chachu yoyote au asali katika sadaka inayotolewa kwa Mwenyezi Mungu kwa moto. 12 Unaweza kuzileta kwa Mwenyezi Mungu kuwa sadaka ya malimbuko, lakini haziwezi kutolewa juu ya madhabahu kama harufu nzuri ya kupendeza. 13 Koleza sadaka zako zote za nafaka kwa chumvi. Usiache kuweka chumvi ya agano la Mungu wako katika sadaka zako za nafaka; weka chumvi kwenye sadaka zako zote.
14 “ ‘Ukileta malimbuko ya sadaka ya nafaka kwa Mwenyezi Mungu, utatoa masuke yaliyopondwa ya nafaka mpya iliyookwa kwa moto. 15 Weka mafuta na uvumba juu yake; ni sadaka ya nafaka. 16 Kuhani atateketeza ile sehemu ya kumbukumbu katika hiyo sadaka ya nafaka iliyopondwa, na mafuta, pamoja na uvumba wote, kuwa sadaka iliyotolewa kwa Mwenyezi Mungu kwa moto.