Zaburi 11
Kumtumaini Mwenyezi Mungu
Kwa mwimbishaji. Zaburi ya Daudi.
1 Kwa Mwenyezi Mungu ninakimbilia.
Unawezaje basi kuniambia:
“Ruka kama ndege utorokee kwenye mlima wako.
2 Hebu tazama, waovu wanapinda nyuta zao;
wanaweka mishale kwenye nyuzi zake
ili wakiwa gizani, wawapige
walio wanyofu wa moyo.
3 Wakati misingi imeharibiwa,
mwenye haki anaweza kufanya nini?”
4 Mwenyezi Mungu yuko ndani ya Hekalu lake takatifu;
Mwenyezi Mungu yuko kwenye kiti chake cha enzi mbinguni.
Huwaangalia wana wa watu,
macho yake yanawachunguza.
5 Mwenyezi Mungu huwachunguza wenye haki,
lakini nafsi yake inachukia waovu
na wale wanaopenda mapigano.
6 Atawanyeshea waovu makaa ya moto mkali
na kiberiti kinachowaka;
upepo wenye joto kali ndio fungu lao.
7 Kwa kuwa Mwenyezi Mungu ni mwenye haki,
yeye hupenda haki.
Wanyofu watauona uso wake.