Zaburi 16
Sala ya matumaini 
 Utenzi wa Daudi. 
  1 Ee Mungu, uniweke salama,  
kwa maana kwako nimekimbilia.   
 2 Nilimwambia Mwenyezi Mungu, “Wewe ndiwe Bwana wangu;  
pasipo wewe sina jambo jema.”   
 3 Kuhusu watakatifu walio duniani,  
hao ndio wenye fahari,  
na ninapendezwa nao.   
 4 Huzuni itaongezeka kwa wale  
wanaokimbilia miungu mingine.  
Sitazimimina sadaka za damu kwa miungu kama hiyo,  
au kutaja majina yao mdomoni mwangu.   
 5 Mwenyezi Mungu umeniwekea fungu langu na kikombe changu;  
umeyafanya mambo yangu yote yawe salama.   
 6 Alama za mipaka zimeniangukia mahali pazuri,  
hakika nimepata urithi mzuri.   
 7 Nitamsifu Mwenyezi Mungu ambaye hunishauri,  
hata wakati wa usiku moyo wangu hunifundisha.   
 8 Nimemweka Mwenyezi Mungu mbele yangu daima.  
Kwa sababu yuko mkono wangu wa kuume,  
sitatikisika.   
 9 Kwa hiyo moyo wangu unafurahia,  
na ulimi wangu unashangilia;  
mwili wangu nao  
utapumzika salama,   
 10 kwa maana hutaniacha Kuzimu*Kuzimu kwa Kiebrania ni Sheol, yaani Shimo lisilo na mwisho.,  
wala hutamwacha Mtakatifu Wako  
kuona uharibifu.   
 11 Umenijulisha njia ya uzima;  
utanijaza na furaha mbele zako,  
pamoja na furaha ya milele  
katika mkono wako wa kuume.