Zaburi 15
Kitu Mwenyezi Mungu anachotaka 
 Zaburi ya Daudi. 
  1 Mwenyezi Mungu, ni nani awezaye kukaa  
katika Hekalu lako?  
Nani awezaye kuishi  
katika mlima wako mtakatifu?   
 2 Ni yule aendaye pasipo mawaa,  
atendaye yaliyo haki,  
asemaye kweli toka moyoni mwake,   
 3 na hana masingizio ulimini mwake,  
asiyemtenda jirani yake vibaya,  
na asiyemsingizia mwenzake,   
 4 ambaye humdharau mtu mbaya,  
lakini huwaheshimu wale wamwogopao Mwenyezi Mungu,  
yule atunzaye kiapo chake  
hata kama anaumia.   
 5 Yeye akopeshaye fedha yake bila riba,  
na hapokei rushwa dhidi ya mtu asiye na hatia.  
Mtu afanyaye haya  
kamwe hatatikisika.