Zaburi 14
Uovu wa wanadamu
(Zaburi 53)
Kwa mwimbishaji. Zaburi ya Daudi.
1 Mpumbavu anasema moyoni mwake,
“Hakuna Mungu.”
Wamepotoka, matendo yao ni maovu kabisa;
hakuna hata mmoja atendaye mema.
2 Mwenyezi Mungu anawachungulia wanadamu
kutoka mbinguni
aone kama kuna mwenye hekima,
yeyote anayemtafuta Mungu.
3 Wote wamepotoka,
wote wameoza pamoja;
hakuna atendaye mema,
naam, hakuna hata mmoja!
4 Je, watendao maovu kamwe hawatajifunza:
wale ambao huwala watu wangu
kama watu walavyo mkate,
hao ambao hawamwiti Mwenyezi Mungu?
5 Wako hapo, wameingiwa na hofu kuu,
maana Mungu yupo pamoja na wenye haki.
6 Ninyi watenda maovu mnakwamisha mipango ya maskini,
bali Mwenyezi Mungu ndiye kimbilio lao.
7 Laiti wokovu wa Israeli
ungekuja kutoka Sayuni!
Mwenyezi Mungu anaporejesha
wafungwa wa watu wake,
Yakobo na ashangilie,
Israeli na afurahi!