Zaburi 14
Uovu wa wanadamu 
 (Zaburi 53)  
Kwa mwimbishaji. Zaburi ya Daudi. 
  1 Mpumbavu anasema moyoni mwake,  
“Hakuna Mungu.”  
Wamepotoka, matendo yao ni maovu kabisa;  
hakuna hata mmoja atendaye mema.   
 2 Mwenyezi Mungu anawachungulia wanadamu  
kutoka mbinguni  
aone kama kuna mwenye hekima,  
yeyote anayemtafuta Mungu.   
 3 Wote wamepotoka,  
wote wameoza pamoja;  
hakuna atendaye mema,  
naam, hakuna hata mmoja!   
 4 Je, watendao maovu kamwe hawatajifunza:  
wale ambao huwala watu wangu  
kama watu walavyo mkate,  
hao ambao hawamwiti Mwenyezi Mungu?   
 5 Wako hapo, wameingiwa na hofu kuu,  
maana Mungu yupo pamoja na wenye haki.   
 6 Ninyi watenda maovu mnakwamisha mipango ya maskini,  
bali Mwenyezi Mungu ndiye kimbilio lao.   
 7 Laiti wokovu wa Israeli  
ungekuja kutoka Sayuni!  
Mwenyezi Mungu anaporejesha  
wafungwa wa watu wake,  
Yakobo na ashangilie,  
Israeli na afurahi!