Zaburi 13
Sala ya kuomba msaada
Kwa mwimbishaji. Zaburi ya Daudi.
1 Hadi lini, Ee Mwenyezi Mungu? Je, utanisahau milele?
Utanificha uso wako hadi lini?
2 Nitapambana na mawazo yangu hadi lini,
na kila siku kuwa na majonzi moyoni mwangu?
Adui zangu watanishinda hadi lini?
3 Nitazame, unijibu, Ee Mwenyezi Mungu, Mungu wangu.
Yatie nuru macho yangu,
ama sivyo nitalala usingizi wa mauti.
4 Adui yangu atasema, “Nimemshinda,”
nao adui zangu watashangilia nitakapoanguka.
5 Lakini ninategemea upendo wako usiokoma;
moyo wangu unashangilia katika wokovu wako.
6 Nitamwimbia Mwenyezi Mungu,
kwa kuwa amekuwa mwema kwangu.