Zaburi 20
Maombi kwa ajili ya ushindi
Kwa mwimbishaji. Zaburi ya Daudi.
1 Mwenyezi Mungu na akujibu unapokuwa katika dhiki,
jina la Mungu wa Yakobo na liwe kinga yako.
2 Na akutumie msaada kutoka patakatifu
na akupatie msaada kutoka Sayuni.
3 Na azikumbuke dhabihu zako zote,
na azikubali sadaka zako za kuteketezwa.
4 Na akujalie haja ya moyo wako,
na aifanikishe mipango yako yote.
5 Tutashangilia kwa furaha utakaposhinda,
tutainua bendera zetu kwa jina la Mungu wetu.
Mwenyezi Mungu na akupe haja zako zote.
6 Sasa nafahamu kuwa Mwenyezi Mungu
humwokoa mpakwa mafuta wake,
humjibu kutoka mbingu yake takatifu
kwa nguvu za wokovu wa mkono wake wa kuume.
7 Wengine wanatumaini magari ya vita, na wengine farasi,
bali sisi tutalitumainia jina la Mwenyezi Mungu, Mungu wetu.
8 Wao wameshushwa chini na kuanguka,
bali sisi tunainuka na kusimama imara.
9 Ee Mwenyezi Mungu, mwokoe mfalme!
Tujibu tunapokuita!